The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on April 20, 2024. Register Here

Search
Close this search box.

Headlines

Serikali yaunda kamati sakata la kikokotoo cha pensheni kwa wastaafu
Habari Kubwa Leo, Mei 6, 2024
Kimbunga Hidaya Sababu Upepo Mkali na Mvua Zinazoendelea Maeneo ya Pwani
Habari kubwa Leo Mei 3, 2024
Habari kubwa Leo Mei 2, 2024
Habari kubwa leo Aprili 29, 2024
Habari Kubwa Leo Aprili 24, 2024
Habari Kubwa Leo Aprili 23, 2024

Live Reporting

Habari Kubwa Leo Mei 7, 2024

Serikali imeunda kamati ya kukusanya na kuchambua maoni na mapendekezo ya viwango vya nyongeza ya pensheni ili kuwezesha maandalizi ya rasimu ya waraka wa Baraza la Mawaziri kuhusu nyongeza ya pensheni kwa wastaafu wanaolipwa na Hazina. 

Hayo yamesemwa leo Mei 7, 2024, bungeni jijini Dodoma, na Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, wakati akijbu swali la mbunge wa viti maalumu kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taska Restuta Mbongo, aliyetaka kufahamu mikakati ya Serikali juu ya malalamiko ya kikokotoo cha pensheni kwa wastaafu.

Nchemba emeongeza kuwa taarifa ya kamati hiyo na kazi ya uchambuzi wa maoni pamoja na mapendekezo ya wadau inatarajiwa kukamilika kabla ya Juni 30, 2024.

Katika siku za hivi karibuni kumekuwa na malalamiko ya wafanyakazi na wadau juu ya kikokotoo kipya katika mifuko ya hifadhi ya jamii kilichoanza kutumika Julai 1, 2022, kutokana na malipo ya wastaafu ya mkupuo kupungua kutoka asilimia 50 mpaka asilimia 33, kitu ambacho watu hao wameonekana kutokiunga mkono. 

Zaidi ya Shilingi bilioni 11 zalipwa na Serikali kwa wananchi walioathiriwa na wanyama

Serikali imelipa zaidi ya bilioni 11 kama kifuta jasho na kifuta machozi kuanzia mwaka wa fedha 2017/2018 hadi Machi, 2024 kwa wananchi waliothirika na changamoto mbalimbali za wanyama wakali na waharibifu.

Taarifa hiyo imetolewa leo Mei 7, 2024, bungeni jijini Dodoama, na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Dunstan Kitandula, wakati akijibu swali la mbunge wa viti maalumu kupitia CHADEMA, Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, aliyetaka kufahamu katika kipindi cha mwaka 2017 hadi mwaka 2022 ni kiasi gani cha fedha kimelipwa kama kifuta jasho kwa waathirika wa uharibifu wa mazao na mauaji yaliyofanywa na tembo.

Kitandula ameongeza kuwa Wizara ya Maliasili na Utalii tayari imezifanyia marekebisho kanuni za kifuta jasho na machozi, na sasa ipo katika hatua za mwisho za majadiliano na Wizara ya Fedha ili kupata ridhaa ya matumizi ya viwango vipya vya fidia kwa kuwa viwango vilivyopo sasa vimepitwa na wakati.

Uharibifu mkubwa wa mazao na mauaji hapa nchini yamekuwa yakifaywa na wanayama wa porini aina ya tembo. Baadhi ya maeneo ambayo yamekuwa yakishuhudia changamoto hii ni wilaya za Liwale na Nachingwea huko mkoani Lindi, lakini wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma pamoja wilaya ya Handeni iliyopo mkoani Tanga.

Serikali kuongeza idadi wa wanafunzi wanaopata mikopo ya elimu ya juu

Serikali imesema itaongeza fursa za utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu kutoka wanafunzi 223,201 hadi 252,245 kwa mwaka 2024/2025 ili kuwezesha na kuimarisha huduma ya utoaji na upatikanaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu wenye sifa na uhitaji.

Hayo yamebainishwa na  Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda,  leo Mei 7, 2024, bungeni jijini Dodoma, wakati akiwasilisha hotuba yake ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Wizara yake kwa mwaka 2024/2025.

Akifafanua namna ya utolewaji wa mikopo hiyo, Profesa Mkenda amesema kuwa Serikali itatoa mikopo kwa wanafunzi 84,500 wa mwaka wa kwanza ambapo shahada ya kwanza itahusisha wanafunzi 80,000, shahada za juu zitahusisha wanafuzni 2,000, wanaosoma nje ya nchi itakuwa wanafunzi 500, udhamanini wa masomo wa Samia utahusisha wanafunzi 2,000 na pia itatoa mikopo kwa wanafunzi 157,745 wanaoendelea na masomo.

Habari Kubwa Leo, Mei 6, 2024

Serikali kumtafuta mwekezaji mwingine bandari ya Dar.

Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, amesema Serikali inaendelea na utaratibu wa kumpata muwekezaji mwingine katika bandari ya Dar es Salaam atakayekuwa anafanya shughuli za uendeshaji kuanzia gati namba nane hadi 11 kwa lengo la kuongeza tija katika bandari hiyo. 

Profesa Mbarawa ameyasema hayo leo Mei 6, 2024, bungeni jijini Dodoma, wakati akiwasilisha Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka 2024/2025.   

Profesa Mbarawa ameongeza kuwa utaratibu huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kushirikisha sekta binafsi katika kuiendesha bandari hiyo mara baada ya kukamilika kwa mchakato wa kukabidhi kwa muwekezaji uendeshaji wa gati namba nne hadi saba. 

Suala la kuwapa wawekezaji binafsi uendashaji wa bandari ya Dar es Salaam limekuwa likipingwa vikali na wadau mbalimbali hapa nchini. Oktoba 22, 2023, Tanzania ilisaini mikataba mitatu ya uendeshaji wa bandari ya Dar es Salaam kwa muda wa miaka 30 na kampuni ya Dubai ya DP World licha ya kuwepo kwa ukinzani mkali dhidi ya mpango huo. 

Godlisten Malisa na Boniface Jacob wafikishwa mahakamani 

Meya wa zamani wa Ubungo, Boniface Jacob na mwanaharakati Godlisten Malisa, wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kujibu tuhuma zinazowakabili za uchochezi na kuchapisha taarifa za uongo kinyume na sheria. 

Washtakiwa hao wamefikishwa mahakamani leo Mei 6, 2024, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Ushindi Swallo, ambapo kwa mujibu wa Wakili wa Serikali, Neema Moshi, amesema wawili hao wameshtakiwa chini ya kifungu cha 16 cha Sheria ya Makosa ya Kimtandao namba 14 ya mwaka 2015. 

Baada ya kusomewa mashtaka hayo kesi hiyo imeairishwa mpaka Juni 6, 2024, na wawili hao wameachiwa kwa dhamana baada ya kila mmoja kusaini bondi ya Shilingi milioni mbili. 

Jacob na Malisa waliachiliwa kwa dhamana na Jeshi la Polisi Aprili 27, 2024, baada ya kushikiliwa kwa siku tatu katika vituo mbalimbali vya polisi. Kushikiliwa kwao kulihusishwa na taarifa walioichapisha kwenye mitandao ya kijamii mnamo Aprili 13, 2024, kuhusu kupotea kwa kijana aliyefahamika kama Robert Mushi.

Aprili 23, 2024 Jeshi la Polisi kanda ya Dar es Salaam lilitoa taarifa kuwa Mushi alifariki kwa ajali na mwili wake kuhifadhiwa Hospitali ya Polisi, habari iliyozua mjadala mitandaoni. Taarifa hiyo pia ilitoa wito kwa Jacob na Malisa kuripoti polisi kwa kile kilichodaiwa wanasambaza taarifa za uongo.

Polisi wawashikilia watu 10 kwa tuhuma za kujihusisha na mikopo ya ‘kausha damu’ 

Watu 10 wanashikiliwa na Jeshi la Polisi katika mikoa ya Songwe na Mtwara kwa tuhuma za kujihusisha na utoaji wa mikopo ya kausha damu ambapo wanatarijiwa kufikishwa mahakamani baada ya upelelezi kukamilika. 

Akizungumza na waandishi wa habari leo Mei 6, 2024, Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Songwe, Augustino Senga, amesema wamewakamata watu sita kwa kufanya biashara ya kutoa mikopo bila ya kuwa na leseni kinyume cha Sheria ya Mikopo Midogo Namba 10 ya mwaka 2018, Kifungu cha 16.

Naye Kamanda wa Polisi mkoani Mtwara, Issa Juma Suleiman, amewaambia waandishi wa habari kuwa wanawashikilia watu wanane kutoka kampuni za Mloganile Microfinance, Soulmate General Supplier Ltd pamoja na Joma Microfinance Company Ltd kwa tuhuma za kujihusisha na kosa kama hilo.

Hivi karibuni bungeni ulizuka mjadala juu ya mikopo kausha damu inayotolewa na baadhi ya taasisi za fedha rasmi na zisizo rasmi.

Mikopo hiyo ilielezwa kuwa inatesa wananchi, hivyo Serikali iliahidi kuchukua hatua za kisheria na kuona namna bora ya utolewaji wa mikopo hiyo.

Kimbunga Hidaya Sababu Upepo Mkali na Mvua Zinazoendelea Maeneo ya Pwani

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesema kuwa uwepo wa kimbunga Hidaya maeneo ya karibu na pwani kimepelekea vipindi vya upepo mkali na mvua maeneo tofauti tangu jana.

Kwa mujibu wa taarifa ya TMA hadi kufika saa tisa usiku wa kumkia leo, kimbunga hiko kilikuwa umbali wa kilomita 125 kutoka pwani ya Kilwa (Mkoa wa Lindi), Kilomita 93 kutoka Pwani ya Mafia  na kilomita 128 kutoka pwani ya Dar es Salaam kikiwa na kasi ya upepo inayofikia kilomita 120 kwa saa.

Hali hii imepelekea kuwepo kwa mvua kubwa juu ya wastani katika maeneo ya mkoa wa Mtwara na Lindi, huku maeneo ya Dar es Salaam, Mtwara, Kilwa na Zanzibar yakishuhudia upepo mkali unaoenda kilomita 50 kwa saa.

TMA imeeleza kuwa kimbunga HIDAYA kitaendelea kusogelea maeneo ya pwani na kinatarajiwa kupungua nguvu kuelekea usiku wa Mei 5, 2024. Hivyo wananchi wametakiwa kuchukua tahadhari.

Habari kubwa Leo Mei 3, 2024

Serikali yaahidi kuimarisha ulinzi na usalama kwa waandishi wa habari

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa,  amesema kuwa Serikali itaendelea kuimarisha ulinzi na usalama wa waandishi wa habari ili kuhakikisha kwamba wanafanya kazi zao pasipo kusumbuliwa mahali popote wanatakapokuwa wakitekeleza majukumu yao.  

Majaliwa ameyasema hayo leo Mei 3, 2024, wakati alipokuwa akizungumza kama mgeni rasmi kwenye siku ya kilele cha maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari yaliyofanyika huko jijini Dodoma.  

Kauli hiyo ya Majaliwa imekuja kufuatia taarifa iliyotolewa na Rais wa Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC), Deogratius Nsokolo, ambaye katika hotuba yake alieleza kwamba, bado waandishi wa habari nchini wanakumbana na changamoto kutolewa vitisho, kupigwa na kuachwa kwenye misafara wakati wakitafuta habari. 

Akieleza juu ya ufumbuzi wa baadhi ya changamoto hizo, Majaliwa amewataka watendaji wa ofisi za Serikali kuhakikisha kuwa wanaandaa magari kwa ajili ya waandishi wa habari kwenye kila ziara ya kiongozi wa Serikali ili kupunguza usumbufu ambao waandishi wa habari wamekuwa wakikutana nao.

Serikali yawataka wananchi kuchukua tahadhari dhidi ya kimbunga Hidaya

Serikali imezielekeza mamlaka za mikoa iliyotajwa kuwa katika hatarini kukumbwa na kimbunga Hidaya kuchukua tahadhari na kutoa taarifa kuhusu mwenendo wa kimbunga hicho pale ambapo dalili za uwepo wake zitakapojitokeza. 

Akizungumza bungeni leo Mei 3, 2024, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Jenista Mhagama, amewataka pia wananchi ambao wanafanya shughuli zao katika maeneo ya kando ya bahari wachukue tahadhari na kuendelea kufuatilia taarifa za Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) zinazohusiana na kimbunga hicho. 

Mei 2, 2024, TMA ilieleza kuwa mwenendo wa mifumo ya hali ya hewa baharini inaonesha kuwa kuna uwezekano mkubwa wa kimbunga Hidaya kusogea karibu kabisa na Pwani ya Tanzania na kitaendelea kuwepo hadi Mei 6, 2024.  

Baadhi ya maeneo ya mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani (ikijumuisha visiwa vya Mafia), Dar es Salaam, Tanga, Morogoro, visiwa vya Unguja na Pemba yalielezwa kuwa hatarini kuathirika na kimbunga hicho. 

Idadi ya watu waliofariki kutokana na mvua za El-Nino yafikia 161

Msemaji Mkuu wa Serikali, Mobhare Matinyi, leo Mei 3, 2024, amewaambia waandishi wa habari jijini Dodoma kuwa idadi ya watu waliofariki kutokana na mvua za El-Nino kuanzia mwezi Oktoba 2023 imefikia watu 161.

Matinyi ameongeza kuwa idadi ya watu waliojeruhiwa imefikia watu 250 na kaya 52,000 zenye zaidi ya watu 210,000 zimeathirika kutokana na mvua hizo huku nyumba zaidi ya 15,000 pia zikiharibiwa. 

Maeneo ambayo Matinyi amesema kuwa yameathirika na mvua hizo ni pamoja na Pwani, Morogoro, Mbeya, Iringa, Tabora, Dodoma, Lindi, Mtwara, Arusha, Kagera, Shinyanga, Geita, Songwe, Rukwa pamoja na Manyara.

Taarifa iliyowahi kutolewa na Mamlaka ya Utabiri wa Hali ya Hewa (TMA) ilibainisha uwepo kwa mvua kubwa kuanzia mwezi Oktoba 2023 hadi Mei 2024 katika maeneo mbalimbali nchini. 

Mwezi Oktoba hadi Desemba 2023, kulikuwa na ongezeko  la mvua ambapo jumla ya milimita 534.5 zilipimwa ikilinganishwa na milimita 227.2 kwa mwaka 2022 ikiwa ni ongezeko la asilimia 135.

Habari kubwa Leo Mei 2, 2024 

Kimbunga HIDAYA kuisogelea pwani ya Tanzania  

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesema kuwa mwenendo wa mifumo ya hali ya hewa baharini inaonesha kuwa kuna uwezekano mkubwa wa kimbunga Hidaya kusogea karibu kabisa na Pwani ya Tanzania kuanzia usiku wa leo, Mei 2, 2024, na kitaendelea kuwepo hadi Mei 6, 2024.  

Taarifa ya TMA iliyotolewa leo Mei 2, 2024, imeeleza kuwa baadhi ya maeneo ya mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani (ikijumuisha visiwa vya Mafia), Dar es Salaam, Tanga, Morogoro, visiwa vya Unguja na Pemba yanaweza kuathirika na hali hiyo, kwa kukubwa na vipindi vya mvua na upepo mkali.  

TMA imeshauri wananchi katika maeneo tajwa wanaojihusisha na shughuli mbalimbali baharini kuchukua tahadhari kubwa ili kujiepusha na madhara yanayoweza kuletwa na kimbunga hicho.  

Mauzo ya nje ya mazao ya chakula yafikia dola bilioni 2.3

Serikali imesema kuwa kwa mwaka wa fedha 2022/2023 mauzo ya mazao ya chakula nje ya nchi yamefikia dola za Kimarekani bilioni 2.3, ikilinganishwa dola za Kimarekani bilioni 1.2 zilizopatikana mwaka 2019/2020.  

Hayo yamesemwa leo Mei 2, 2024, bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe, wakati akiwasilisha Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Wizara ya Kilimo kwa mwaka 2024/2025.  

Bashe ameongeza kuwa uzalishaji wa mazao ya chakula katika msimu wa mwaka 2022/2023 ulifika tani milioni 20.4, ikilinganishwa na tani milioni 17.1 zilizopatikana msimu wa mwaka 2021/2022, ambalo ni sawa na ongezeko la asilimia 19. 

Aidha, amesema uzalishaji wa mazao ya nafaka ulikua kwa asilimia 11.6  na yasiyo ya nafaka uliongeza kwa asilimia 8.9, hali ambayo ilifanya utoshelevu chakula nchini kufikia asilimia 120 ukilinganisha na utoshelevu wa asilimia 114 uliokuwepo kwa mwaka wa fedha 2021/2022.  

Sekta ya kilimo imeendelea kuwa mhimili mkubwa wa uchumi kwa kuchangia kiasi kikubwa kwenye pato la taifa na kutoa ajira kwa wananchi wengi. Kwa mwaka 2023 sekta hiyo ilichangia asilimia 26.5 kwenye pato la taifa na ikatoa ajira kwa asilimia 65.6 huku ikiwa imechangia asilimia 65 ya malighafi zote za viwanda.

Sheria ya Sukari kufanyiwa marekebisho kuwawezesha NFRA kununua na kuhifadhi sukari

Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe, amesema kuwa Serikali inapanga kufanya marekebisho katika Sheria ya Sukari namba sita ya mwaka 2001 kwenye sheria ya fedha ya mwaka 2024, ili kumuwezesha Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) kununua na kuhifadhi sukari kwenye hifadhi ya taifa ya chakula. 

Mpango huo umeelezwa kuwa utaenda pamoja na marekebisho ya kanuni za NFRA yatakayoiweka sukari iwe sehemu ya usalama wa chakula. 

Hayo yamesemwa leo Mei 02, 2024, bungeni jijini Dodoma, wakati Bashe alipokuwa akiwasilisha Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka 2024/2025.  

Mwishoni mwa mwaka jana na mwanzoni mwa mwaka huu Tanzania ilishuhudia upungufu mkubwa wa sukari, hali ambayo ilipelekea bidhaa hiyo kuuzwa kwa bei ya juu. 

Wananchi walilazimika kununua kilo moja ya bidhaa hiyo kwa Shilingi 4,000 hadi 5,000 kutoka Shilingi 2,800 hadi Shilingi 3,000 iliyokuwa imezoeleka. 

Ili kutatua tatizo hili, Serikali ililazimika kutoa vibali kwa wafanyabiashara ili waagize sukari tani 50,000 kutoka nje ya nchi kwa ajili ya kupambana na upungufu uliokuwepo.

Habari kubwa leo Aprili 29, 2024

TRA yakusanya kodi Shilingi bilioni 12 kutoka kampuni za nje ikiwemo Google 

Kwa mara ya kwanza Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) hadi kufikia Machi 2024 imekusanya kodi Shilingi bilioni 12 kutoka kampuni zinazofanya kazi Tanzania lakini hazina ofisi mama nchini ikiwamo kampuni ya Marekani ya Google LLC. 

Taarifa hiyo imetolewa leo Aprili 29, 2024, jijini Dodoma na Kaimu Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi wa TRA, Hudson Kamoga, muda mfupi baada ya kuwasilisha mada katika mkutano mkuu wa 13 wa Kitaaluma wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) unaohudhuriwa na wanachama zaidi ya 150. 

Kamoga amesema kodi hiyo imekusanywa baada ya kupitishwa kwa Sheria ya Fedha ya mwaka 2023 na akazitaja kampuni zingine za mtandaoni ambazo kwa mujibu wa sheria hiyo zinapaswa kulipa kodi hiyo na zimeanza kulipa kuwa ni Tiktok, Facebook na Netflix.

Serikali kuanza kulipa madeni ya vyombo vya habari ya zaidi ya bilioni 18

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye, amesema kuwa Serikali imeanza kufanya mipango ya kulipa deni la zaidi ya bilioni 18 inayodaiwa na vyombo mbalimbali vya habari hapa nchini.

Nnauye ameyasema hayo leo Aprili 29, 2024, katika mkutano mkuu wa 13 wa mwaka wa kitaaluma wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) unaoendelea jijini Dodoma. 

Kiongozi huyo amesema kati ya Shilingi bilioni 18 zinazodaiwa, Shilingi bilioni tano ni deni kutoka kwenye halamashauri ambazo hazioneshi dalili za kupunguza au kulipa deni hilo na kiasi kinachobakia ni deni kutoka kwenye taasisi za Serikali. 

Kwa upande wake, Naibu Waziri Mkuu, Doto Biteko, ameeleza kuwa Serikali ina dhamira ya dhati kulipa madeni hayo ili kuepuka kudhoofisha vyombo vya habari. Aidha, amewataka wanaodaiwa kutoa taarifa za kina kuhusu deni hilo ili hatua za kulipa ziweze kuchukuliwa haraka.  

Mbunge ataka adhabu ya kifo iondolewe kwa sababu haitekelezwi

Mbunge wa viti maalumu kupitia Chama cha Mapinduzi Shally Raymond ameishauri Serikali ipeleke muswada bungeni kwa ajili ya kuiondoa adhabu ya hukumu ya kifo kwa sababu imekuwa haitekelezwi kwa muda wa takribani miaka 30 sasa. 

Shally amependekeza suala hilo leo Aprili 29, 2024, wakati akichangia hoja mara baada ya kuwasilishwa kwa hotuba ya Waziri Katiba na Sheria, Pindi Chana, kuhusu Mpango wa Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara hiyo kwa mwaka 2024/2025.

Kwa mujibu wa Shally hukumu hiyo imekuwa ikiwaweka mahabusu watu waliohukumiwa kunyongwa kwa muda wa miaka 10 hadi 20 pasipo kutekelezwa, kitu ambacho anadai kuwa si haki. 

Ripoti ya haki za binadamu ya Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) ya mwaka 2023 ilirekodi hukumu 37 za adhabu ya kifo. 

Hukumu hii imekuwa ikipigiwa kelele na wadau mbalimbali kuwa iondolewe kwa sababu mara ya mwisho kutekelezwa ilikuwa ni mwaka 1994, wakati wa utawala wa Hayati Ally Hassan Mwinyi.