The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on April 20, 2024. Register Here

Search
Close this search box.

CHADEMA yaanza wiki ya maandamano nchi nzima

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimeanza wiki ya maandamano ya amani yatakayofanyika mikoa mbalimbali hapa nchini kuanzia leo Aprili 22,  hadi 30,2024 ikiwa ni utekelezaji wa azimio la Mtwara.

Maandamano hayo yameanzia Bukoba, mkoani Kagera leo tarehe 22 Aprili 2024, ambapo mwenyekiti wa Chama Taifa  Freeman Mbowe ameongoza maandamano hayo ikiwa ni awamu ya kwanza kati ya awamu mbili zitakazofanyika.

Kituo kinachofuata ni mkoa wa Shinyanga ambapo maandamano yatafanyika Wilaya ya Kahama kesho tarehe 23 Aprili 2024 huku ikielezwa kuwa Tundu Lissu yeye ataongoza maandamano mkoani Arusha tarehe 25 Aprili 2024. 

Lengo la CHADEMA kuandamana ni kupinga miswada ya uchaguzi iliyopitishwa bungeni hivi karibuni, kuishinikiza Serikali irejeshe mchakato wa Katiba Mpya pamoja kuitaka Serikali ishughulikie masuala mbalimbali yanayosababisha kuongezeka kwa gharama za maisha.

Makonda afika Dodoma kuhojiwa na Kamati ya Maadili ya Chama.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Paul Makonda amewasili kwenye ofisi za Makao Makuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) jijini Dodoma kwa ajili ya kuhojiwa na Kamati ya Maadili.

Makonda ameitikia wito wa kufika mbele ya kamati hiyo kwa barua aliyoandikiwa Aprili 16, 2024 huku sababu za kuitwa kwake zikiwa hazijawekwa wazi.

Awali, Makonda alitakiwa kufika mbele ya kamati hiyo Aprili 20, 2024 kabla ya kusogezwa mbele na kupangwa kufanyika leo Jumatatu, Aprili 22, 2024.

Lakini, wito huo huenda unahusishwa na kauli ya Makonda aliyoitoa wakati wa kumbukumbu ya miaka 40 ya kifo cha Waziri mkuu wa zamani, Edward Sokoine ambapo Makonda alidai kuwa viongozi wakiwemo mawaziri wamekuwa wakilipa watu kumtukana Rais Samia Suluhu Hassan kwenye mitandao ya kijamii.

Makonda alitoa onyo kwa viongozi hao akisema kama wakiendelea atawataja hadharani na kwamba, hayuko tayari kuona Rais Samia akitukanwa.

Mali za watuhumiwa wa dawa za kulevya Zanzibar kutaifishwa

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Zanzibar (ZDCE), imetangaza kutaifisha mali za watuhumiwa wa dawa za kulevya zenye thamani ya Sh15.3 bilioni kuwa mali ya Serikali.

Akizungumza kuhusu kutaifishwa kwa mali hizo ofisini kwake leo Jumatatu  Aprili 22, 2024 , Kamishna Kanali Burhani Zuberi Nassoro amesema dawa hizo ziliingizwa nchini na wafanyabiashara wakubwa wa dawa za kulevya.

Kamishna Nassoro amewataja watuhumiwa hao kuwa ni Salehe Khamis Basleman na Gawar Bachi Fakir wote wakazi wa Chukwani, Wilaya ya Magharibi B Mkoa wa Mjini Magharibi.

Watuhumiwa hao wamebainika kufanya biashara haramu ya dawa za kulevya Zanzibar, Tanzania Bara, Afrika, Asia, Ulaya na Marekani. Hata hivyo ameleeza kuwa iwapo kuna mtu hajaridhika na tamko hilo anaweza kwenda mahakamani ndani ya siku 30 kuanzia leo.