The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on April 20, 2024. Register Here

Search
Close this search box.

Barabara ya Jangwani, Dar es Salaam yafungwa kutokana na mafuriko

Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART) amesema kuanzia leo Aprili 23, 2024, amesitisha mabasi yake kupita katika barabara ya Jangwani jijini Dar es Salaam mara baada ya barabara hiyo kufungwa kutokana na mafurikio yaliyotokea jijini hapa.

Taarifa iliyotolewa na DART leo Aprili 23, 2024, imesema kuwa huduma ya usafiri wa mabasi yanayotoka Kimara hadi Kivukoni na Gerezani zitaishia katika kituo cha Magomeni Mapipa. 

Aidha, taarifa hiyo imesema huduma za mabasi zitaendelea kutolewa kama kawaida kwa njia ya Morroco kwenda Kimara na eneo la katikati mwa jiji kwa njia ya Muhimbili na Gerezani. 

Eneo la Jangwani ni eneo ambalo kwa muda mrefu limekuwa likikumbwa na changamoto ya mafuriko mara tu mvua kubwa zinaponyesha. 

Suluhu ya changamoto hiyo inatarajiwa kuwa ni mradi wa ujenzi wa Bonde la Msimbazi ulioanza mwezi huu kwa hatua za awali. Mradi huo unatarajiwa kuchukua muda wa miaka mitano na utagharimu Shilingi bilioni 675. 

Ujenzi wake utahusisha miundombinu ya kukabiliana na mafuriko, ujenzi wa karakana ya mwendokasi eneo la Ubungo Maziwa, ujenzi wa daraja la Jangwani, ujenzi wa busatani ya jiji na uendelezaji wa maeneo ya makazi na biashara.

Wabunge Zanzibar: Muungano unatupatia kila raha, Serikali itatue kero zinapojitokeza

Baadhi ya wabunge wanaotoka Zanzibar wameeleza kuwa muungano uliopo hivi sasa kati ya Tanganyika na Zanzibar una manufaa makubwa lakini wameitaka Serikali iendelee kutafuta suluhu za changamoto zinazojitokeza. 

Hayo yameelezwa leo Aprili 23, 2024, bungeni, jijini Dodoma, wakati wabunge hao walipokuwa wakichangia mjadala wa bajeti ya Wizara ya Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira. 

Akizungumzia moja ya suala ambalo amehitaji litafutiwe ufumbuzi, mbunge wa viti maalumu anayewakilisha Unguja Kaskazini kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Sada Mansoor, amesema ni usumbufu mkubwa kwa wananchi wa pande hizo mbili wanapotoka upande mmoja na kuingia upande wa pili kupitia bandari ya Dar es Salaam na ile ya Zanzibar. 

Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar unatarajiwa kutimiza miaka 60 hapo Aprili 26, 2024. Muungano huo umekuwa ukikabiliwa na kero kadhaa ambazo wadau mbalimbali wamekuwa wakishinikiza zitafutiwe ufumbuzi. 

Machi 26, 2024, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Selemani Jafo, alisema kuwa kati ya kero 25 za Muungano zilizokuwepo mwaka 2010, Serikali imefanikiwa kutatua kero 22. 

Bandari zisizo rasmi 69 zabainika kuleta athari za kimazingira

Jumla ya bandari zisizo rasmi 69 zimekaguliwa kwa mwaka 2023/2024 na kubaininika kuleta athari za kimazingira ikiwemo kumwaga mafuta ya taa, taka ngumu na kutiririsha maji taka kwenda kwenye maziwa, bahari na uharibifu wa bayoanuai unaotokana na uondoaji wa uoto wa asii.

Haya yameelezwa leo Aprili 23, 2024, bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Selemani Jafo, wakati akiwasilisha hotuba ya ofisi hiyo kuhusu mapitio ya utekelezaji wa mpango wa bajeti kwa mwaka 2023/2024 na makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2024/2025.

Jafo amesema kukabiliana na changamoto hizo, Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) lilizishauri mamlaka zinazohusika na masuala ya bandari kufanya tathmini za mazingira, kutoa elimu kwa wadau, kusimamia Sheria ya Usimamizi wa Mazingira, kuhamasisha jamii kuhifadhi mazingira, kuimarisha miundombinu ya bandari na kubadili maeneo ya kuendeshea bandari hizo.

Kwa mujibu wa Jafo, mamlaka zilizoshauriwa kufanya tathmini hiyo ni Mamlaka ya Bandari Tanzania na Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania.