The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on April 20, 2024. Register Here

Search
Close this search box.

Watu 39 wapoteza maisha kutokana na mafuriko Pwani, Morogoro na Arusha

Watu 39 wamepoteza maisha katika mikoa ya Pwani, Morogoro na Arusha kutokana na mvua kubwa zilizonyesha. Mvua hizo pia zimewaacha maelfu ya watu bila makazi katika maeneo hayo pamoja na kuharibu mashamba ya chakula na miundombinu.  

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Ijumaa ya Aprili 12, 2024, na Msemaji Mkuu wa Serikali, Mobhare Matinyi, katika mkoa wa Morogoro idadi ya watu waliopoteza maisha ni 28 na wengine watano ni kutoka mkoani Pwani. 

Nako mkoani Arusha, mkuu wa mkoa huo, Paul Makonda, ameeleza kuwa mpaka sasa watu sita wamepoteza maisha kutokana na athari za mvua zilizonyesha kuanzia Aprili 8 hadi Aprili 12, 2024. 

Kutokana na matukio hayo, Rais Samia Suluhu Hassan ametoa pole kwa wote waliokumbwa na mafuriko alipokuwa akishiriki misa maalumu ya miaka 40 ya kumbukumbu ya kifo cha Hayati Edward Moringe Sokoine, leo Aprili 12, 2024, akisema kuwa Serikali itakuchukua hatua zote kurejesha utulivu katika mikoa iliyoathirika.

Rais Samia: Hayati Sokoine atakumbukwa kwa uwajibikaji kupitia matendo yake 

Rais Samia Suluhu Hassan ameeleza kuwa Waziri Mkuu wa zamani, Hayati Edward Moringe Sokoine, hautasaulika hapa nchini kwa sababu alikuwa ni kiongozi aliyesisitiza uwajibikaji kupitia mienendo na matendo yake kwenye uongozi.

Rais Samia ameyasema hayo leo Aprili 12, 2024, aliposhiriki misa maalumu ya miaka 40 ya kumbukumbu ya kifo cha kiongozi huyo, tukio ambalo limefanyika Monduli Juu, mkoani Arusha, eneo ambalo lilikuwa ndiyo nyumbani kwake enzi za uhai wake. 

Rais Samia ameeleza kuwa funzo hilo kuu kutoka kwa Sokoine linatokana na umahiri wake katika kazi tatu alizozisimamia kipindi cha uongozi wake ambazo ni kazi ya kusimamia ukombozi kusini mwa Afrika, vita ya Tanzania na Uganda na suala la operesheni uhujumu uchumi. 

Sokoine alikuwa Waziri Mkuu wa Tanzania katika vipindi viwili  Februari 13, 1977 hadi Novemba 7, 1980 na Februari 24, 1983 hadi Aprili 12, 1984. Aliwahi pia kuwa Waziri wa Ulinzi (1972-1977) na Waziri Mdogo wa Mawasiliano, Uchukuzi na Kazi (1967-1972). 

Sokoine anakumbukwa sana katika mapambano yake dhidi ya rushwa na uhujumu uchumi miaka 1980 na alifariki dunia Aprili 12, 1984, kwa ajali ya gari eneo la Wami Dakawa mkoani Morogoro akitokea Dodoma kwenye kikao.

Mradi wa ujenzi wa Bonde la Msimbazi kuanza Aprili 15, 2024

Serikali imesema kuwa mradi wa ujenzi wa Bonde la Msimbazi unaosimamiwa na Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA) utaanza Aprili 15, 2024, kwa hatua ya awali ya ubomoaji wa nyumba zilizopo katika eneo la Jangwani, kandokando mwa mto Msimbazi. 

Akizungumza na waandishi wa habari leo Aprili 12, 2024, jijini Dar es Salaam, Msemaji wa Serikali, Mobhare Matinyi, amesema kuwa TARURA itaanza zoezi la ubomoaji kwa kuzingatia makubaliano yake na wakazi wa eneo hilo, kwamba nyumba zao zilifanyiwa tathimini, wakalipwa fidia, ndipo nyumba husika zitavunjwa. 

Kwa mujibu wa Matinyi hadi kufikia Februari 29, 2024, TARURA ilikuwa imeshaingiza malipo ya fidia ya kiasi cha Shilingi bilioni 52.61 kwenye akaunti za wamiliki wa nyumba 2,155 kati ya wamiliki 2,329 walioandikishwa kwenye daftari la kwanza. 

Mradi wa Bonde la Msimbazi unatarajiwa kuchukua miaka mitano kutoka sasa na utagharimu kiasi cha Shilingi bilioni 675. Ujenzi huo utahusisha miundombinu ya kukabiliana na mafuriko, ujenzi wa karakana ya mwendokasi eneo la Ubungo Maziwa, ujenzi wa daraja la Jangwani, ujenzi wa busatani ya jiji na uendelezaji wa maeneo ya makazi na biashara.