The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on April 20, 2024. Register Here

Search
Close this search box.

Tanzania Yakubali Kulipa Bilioni 237 ya Fidia Kwa Kuvunja Mkataba Mwaka 2018. Yatanguliza Bilioni 92

Katika makubaliano hayo Tanzania itatakiwa kumalizia kiwango kilichobaki kwa awamu mbili, ambapo mpaka Oktoba 24 itatakiwa kulipa dola milioni 25 na ifikapo Machi 30,2025, itatakiwa kulipa dola milioni 30.

subscribe to our newsletter!

Tanzania na kampuni ya uchimbaji madini kutoka Australia, Indiana Resource Limited zimefikia makubaliano ya fidia ambapo Tanzania itailipa kampuni hiyo dola za kimarekani milioni 90 kutokana na kuvunja makubaliano katika Mradi wa Nikeli wa Ntaka Hill uliopo mkoani Lindi. Tanzania imeshatanguliza malipo ya awamu ya kwanza ya dola milioni 35 sawa na bilioni 92.

Haya yameelezwa leo Julai 29,2024 katika taarifa iliyotolewa na kampuni ya Indiana Resouces ambayo inaeleza kuwa kampuni hiyo imekubali kupokea ofa ya Tanzania ya dola milioni 90 sawa na bilioni 237, kiwango ambacho ni kidogo kuliko kile cha awali ambacho Tanzania kiliamriwa kulipa na Kituo cha Kimataifa cha Usuluhishi wa Migogoro ya Uwekezaji (ICSID).

Mnamo Julai 14, 2023, Tanzania ilitakiwa kuilipa kampuni ya Indiana Resources Ltd, dola milioni 109 ambazo ni sawa na takribani shilingi bilioni 250 baada ya kituo hicho kujiridhisha uwepo wa ukiukwaji wa mkataba wa uwekezaji katika Mradi wa Nikeli wa Ntaka Hill.

Kampuni hiyo imeeleza kuwa imeamua kukubali kiwango hicho kupunguza mzigo wa gharama utakaotokana na kuendelea na ubishano katika vyombo mbalimbali vya kisheria. Katika makubaliano hayo Tanzania itatakiwa kumalizia kiwango kilichobaki kwa awamu mbili, ambapo mpaka Oktoba 24 itatakiwa kulipa dola milioni 25 na ifikapo Machi 30,2025, itatakiwa kulipa dola milioni 30.

Changamoto kati ya Indiana Resources na Tanzania ilitokana na mabadiliko ya sheria za madini Tanzania mwaka 2017 na 2018. Mnamo Januari 10, 2018, Serikali ya Tanzania, kupitia Tangazo la Serikali (Government Notice) Namba 01 la mwaka 2018, ilitangaza Kanuni za Haki za Madini za Mwaka 2018, ambazo zilifuta leseni hodhi zilizokwisha tolewa kisheria.

Aidha, Kanuni za Haki za Madini za Mwaka 2018 zilienda mbele zaidi, chini ya kanuni ya 21(2) kwa kueleza kuwa haki zote za madini zilizokuwa zikihodhiwa na wamiliki wa leseni hodhi kwenye maeneo yote yaliyokuwa chini ya leseni hodhi, zitakuwa haki za Serikali ya Tanzania.

Hii iliathiri kampuni ya Indiana Resources iliyokuwa na leseni hodhi katika Mradi wa Nikeli wa Ntaka Hill ,mradi uliokadiriwa na kampuni hiyo kuwa unaweza kupata madini yenye thamani ya dola milioni 217. Leseni hiyo iliyofutwa ilikuwa inategemewa kuisha muda wake mnamo Aprili 2020.

Leseni hodhi ni zile leseni ambazo zinaruhusu kampuni husika kushikilia maeneo kwa kipindi cha leseni bila kufanya chochote ikiwa wana vikwazo vya kiufundi, au hali ya uchumi kutoruhusu.

Msukumo mkubwa wa Tanzania kufuta leseni hodhi ni kile kilichoonekana kuwa ni mfumo wa kinyonyaji ambapo kampuni huweza kushikilia maeneo bila kuyaendeleza huku wakijinufaisha kwa kuweka kama mali katika vitabu vyao ilhali Tanzania ikiwa hainufaiki chochote.

Hata hivyo, kutokufuata taratibu na sheria ilizoziweka kumeweza kuigharimu Tanzania na kujikuta ikifuguliwa mashauri mbalimbali duniani juu ya maamuzi yake katika miaka hiyo.

Digital Freedom and Innovation Day
The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on Saturday April 20, 2024 at Makumbusho ya Taifa.

Register to secure your spot

19 Responses

  1. Mikataba ya aina hiyo hafai sema hata mahakama za,Kimataifa hatendi haki kwani siku zote hulinda makampuni yanayohodhi maeneo hayo. Ni wakati sasa mataifa yenye raslimani kuamka na kuikataa mikataba ya aina hiyo. Tanzania kama nchi haikutendewa haki.

  2. Tanzania ilifanya vizuri katika maamuzi,bora kulipia fidia kuliko kunyonywa na marinading wakati nchi na wananchi hawanufaiki na Mali ya nchi yao

  3. Tunalipa dola za marekani milioni 237, mradi kiujumla una dhamanibya dola za marekani milioni 217. Hivi tutaendelea kweli, ukijaribu kusoma kwa umakini Kwakweli tunaonewa sana hawa wameshikilia eneo bila kufanyia kazi, halafu tunawatupilia mbali wanataka fidia duuh! Tena zaidi ya dhamani ya mradi mzima

    1. Hivi anayetuingiza kwenye mikataba ya kinyonyaji namna hii ni mtanzania na bado yuko hai? TISS ingekuwa inatimiza wajibu wake malipo ya mali zetu wenyewe yasingekuwepo. Mahakama za kimataifa lazima ziwalinde wenzao.

  4. Wanasheria waliohusika kutoa ushauri potofu bila kujali haki ya rasilimali zetu wawajibike kwa matokeo hayo.

  5. Jamani Watanzania tuamke hii mikataba mingine tunabidi tuwaajibishe mrorongo nzima wa watu unakubali mkataba wa kuuza nchi kaa manufaa binafsi haiwezekani mgeni anapewa ardhi yenye madini halafu akatafute mteja ndipo aanze kuchimba mali tunayo lakini hatunufaiki tunazidi kuwa masiki tu. Serekali ibadili sera zake hata katiba kwamba mwekezaji yeyote anayehitaji ardhi badi lazima aingie ubua na Mtanzania mmoja mmoja au kikundi ili kulinda raslimali na kunufaisha wananchi tuwe makini au tutaishia kulalamika tu viongozi fanyeni maamuzi ya taifa siyo ya kujunufaisha

    1. Kwani hiyo Mikataba tunayoingia kama nchi, serikali makini ya CCM inakuwa haina habari? Sasa huo umakini tunao uimba kila siku uko wapi, au ndiyo wanaotuingiza mkenge kila wakati halafu wanawapoteza wanaolalamika kwenye Mitandao?

      1. Unaweza sema ni Kama Kuna Jopo la Wahuni, waliosoma kwa Kodi za Watanzania, wanatengeneza Ajali, kisha wananufaika na huu Uhuni, Haiwezekani kila mara sisi ndio tunaadhibiwa kijinga namna hii, litafutwe shimo la Uhuni huu na Wahuni Tuwakatae kwakupewa adhabu stahiki, ikiwepo hata Kufukuzwa Nchini kama sio Kifungo cha Maisha Haiwezekani Wahuni wachache wakaendelea kutesa Raia Mil. 61. Inauma Inauma Inauma

  6. Ni kweli ilnabidi na sisi watanzabia tuamke tulilala Sana, na pia ifike wakati tujikubali na kujivunia tulionacho kwa apo sasa wasomi wetu au wanasheria wa Tz inamaana hawakuliona ilo awali!!!?

  7. Mbona hawakushtaki kipindi cha Magufuli, wakati huu ndio wanaona sawa kutushtaki, uongozi usio imara unatuponza.

  8. Hii mikataba ingepitiwa yote ya makampuni yanayoshikilia ardhi yetu,huenda kuna watu wananufaika na kesi/fidia hizi.

  9. Tumuombe sana Mwenyezi Mungu siku atokee kiongozi wa nchi ambaye anatambua kuwa nchi yetu Tanzania ni tajiri sana inabidi wananchi wa Tanzania tunufaike na sio kama baadhi ya viongozi wabinafsi wanaowaongoza wageni kunufaika.

  10. Huu ni ujinga na uzembe uliozidi kwani kuandamana sh ngap na aliyekubali kulipa amelipa kwa msingi upi?

  11. Huko nyuma Wahuni walishafanya manyago. Ni busara kwa serikali sasa kuanza kulipa Kwani hakuna namna.
    kuendelea kulumbana muda mrefu deni linaongezeka.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Posts