The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on April 20, 2024. Register Here

Search
Close this search box.

Mabalozi Nchi Kumi Na Sita Watoa Tamko Kuhusu Matukio Ya Utekaji, Kupotea na Mauaji Tanzania

Katika nyakati mbalimbali mabalozi wa nchi za Marekani, nchi za Umoja wa Ulaya, Canada,Norway, Uswisi na Uingereza wametoa matamko kutaka uchunguzi kufanyika juu ya matendo ya kikatili, mauaji, kupotea na utekaji yaliyoshamiri nchini

subscribe to our newsletter!

Leo Septemba 10,2024, mabalozi wa nchi za Umoja wa Ulaya kwa pamoja na mabalozi wa nchi za Canada,Norway, Uswisi na Uingereza wametoa tamko la kuonesha kusikitishwa na matukio ya ukatili, kupotea kwa watu na vifo vya wanaharakati wa kisiasa na haki za kibinadamu nchini Tanzania.

“Tunatoa wito wa kufanyika kwa uchunguzi wa kina kuhusu matukio haya. Tunatoa pole kwa familia zote zilizoathiriwa,” imeeleza taarifa hiyo.

“Tunaihimiza serikali ya Tanzania kuhakikisha ulinzi wa upinzani, kama alivyoahidi Rais Dr. Samia Suluhu Hassan kupitia mpango wake wa ‘4R’, na kwa mamlaka kuchukua jukumu la kulinda haki za msingi za wananchi, ikiwa ni pamoja na uhuru wa kujielekeza,” imeeleza zaidi taarifa hiyo.

Mabalozi hao wameeleza zaidi kuwa wanakaribisha wito wa Rais wa kufanya uchunguzi wa haraka ili kubaini wahalifu waliohusika na kuhakikisha kuwa kuna uwajibikaji. Taarifa ya Mabalozi hawa inakuja siku moja toka Ubalozi wa Marekani kutoa tamko lake jana Septemba 09,2024, tamko liloambatana na salamu za rambirambi kufuatia mauaji ya kiongozi wa CHADEMA, Ali Kibao.

“Marekani inaungana na wale wanaotoa wito wa uchunguzi huru, wa wazi na wa haraka kuhusu utekaji unaoendelea na mauaji ya Ali Mohamed Kibao,” ilieleza sehemu ya tamko hilo.

SOMA: Lema Amweleza Masauni Hatari Anayoiona: ‘Nisaidie Niwepo Kwenye Send-Off ya Mtoto Wangu Akiolewa, Ana Miaka 15’

“Mauaji na kupotea kwa watu, pamoja na kukamatwa, kupigwa, na juhudi nyingine za kuwaengua raia katika uchaguzi zilizotokea mwezi uliopita, havipaswi kuwa na nafasi katika demokrasia. Vitendo hivi vya kikatili vinadhoofisha haki zinazohakikishwa na Katiba ya Tanzania,” ilieleza tamko hilo.

Hivi karibuni kumeibuka matukio mengi ya watu kutekwa, kupotea ikiwemo tukio la hivi karibuni la kutekwa na kuuwawa kwa Ali Kibao. Baadhi ya watu ambao wametekwa au kupotea ambapo The Chanzo iliweza kuongea na wapendwa wao ni pamoja na:

  • Deusdedith Soka (alitekwa Agosti 18,2024)
  • Jacob Godwin Mlay (alitekwa Agosti 18,2024)
  • Frank Mbise (alitekwa Agosti 18,2024)
  • Dioniz Kipanya (alipotea Julai 26,2024)
  • Shadrack Chaula (alitekwa Agosti 02,2024)
  • Enock John Chambala (alipotea Julai 06,2024)
  • James William Sije (Alitekwa Agosti 17,2021)
  • Lilenga Isaya Lilenga (Alipotea Mei 11,2024)
  • Issa Sango (Alipotea Januari 27,2023)
  • Abdulkarim Edimo (Alipotea Januari 27,2023)

Mnamo Agosti 9,2024, Chama cha Mawakili Tanzania kilitoa orodha ya watu 83 iliyoeleza kuwa wametekwa au kupotea nchini Tanzania. Mnamo Septemba 08,2024, Rais Samia Suluhu alitoa taarifa kupitia mtandao wa X ambapo aliagiza vyombo vya uchunguzi kumletea taarifa kuhusu mauaji ya Ali Kibao.

“Nimeagiza vyombo vya uchunguzi kuniletea taarifa ya kina kuhusu tukio hili baya kabisa na mengine ya namna hii haraka. Nchi yetu ni ya kidemokrasia na kila raia ana haki ya kuishi. Serikali ninayoiongoza haivumilii vitendo vya kikatili vya namna hii,” alieleza Rais Samia.

Mwili wa Ali Kibao uliokotwa mnamo Septemba 07,2024, tarehe ambayo wanachama wa CHADEMA hukumbuka tukio la jaribio la kuuwawa kwa Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA, Tundu Lissu, tukio lilolotokea mnamo Septemba 07,2017, ikiwa takribani miaka saba imepita sasa.

Ali Kibao, ambaye alikua ni baba wa watoto sita, anakumbukwa kama kiongozi hodari, mwenye msimamo, na mahusiano mema na watu wengi.

Kibao aliyezikwa jana Septemba 09,2024, huko Tanga, ni mmoja wa Mashujaa wa Vita ya Kagera, baada ya kustaafu utumishi wake Jeshini aliingia katika shughuli za kibiashara na siasa. Kibao amefanya kazi na vyama mbalimbali ikiwemo NCCR, CUF, CCM na mpaka umauti unamfika alikua ni mwanachama na kiongozi wa muda mrefu wa CHADEMA.

Digital Freedom and Innovation Day
The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on Saturday April 20, 2024 at Makumbusho ya Taifa.

Register to secure your spot

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *