The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on April 20, 2024. Register Here

Je, Tumefikiria Kulea Watoto Wanaojali Mazingira?

Tukiwalea watoto wanaojali mazingira, tunawafundisha pia kuwa na huruma, kuwa na maono ya mbali, na kutenda kwa uadilifu.

subscribe to our newsletter!

Watoto wetu ni zawadi, lakini pia ni wajibu mkubwa. Tunapowaangalia wakicheka, wakicheza na kuuliza maswali ya udadisi kuhusu dunia inayowazunguka, tunajiuliza kwa upole: Je, tunawalea kwa namna itakayowawezesha kuilinda dunia yao?

Kesho ya watoto wetu haitakuwa salama kama hawatajifunza kutunza mazingira kuanzia umri mdogo. Na kama wazazi, hatuhitaji kuwa wataalamu wa mazingira na hali ya hewa, au wanaharakati wa mazingira, ili kuanza kuwalea watoto wanaojali mazingira. Safari hii inaanzia pale pale nyumbani kwenye nyumba zetu, bustani zetu, sokoni, kwenye fukwe, na hata njiani tunapowapeleka shuleni.

“Siku moja tulikwenda kufanya usafi mtaani. Tulijitwika mifuko ya plastiki na glovu, tukatembea na watoto, huku tukikusanya taka. Waliniuliza, ‘Mama, kwa nini watu wanatupa chupa barabarani?” Huo ulikuwa mwanzo wa mazungumzo muhimu. Tuliwaeleza kuwa chupa za plastiki hujaza mifereji, huharibu mito, na huchangia vifo vya samaki. Watoto walielewa zaidi kwa sababu waliona kwa macho yao,” mdau mmoja alitueleza.

Kwa hiyo, kama wazazi tunaotaka kufundisha watoto kuhusu mazingira tufanyaje?

Kwanza, tuwafundishe watoto kutotupa taka hovyo. Tunaweza kuweka vyombo vya kutupia taka nyumbani na kuwa na utaratibu wa pamoja wa kuzitupa sehemu sahihi. Tunapokuwa sokoni, au kwenye matembezi, tuwatie moyo wachukue hata kipande cha karatasi kilichoanguka na kukitupa mahali stahiki. Tueleze kwa lugha rahisi kuwa kutunza mazingira ni namna ya kuonesha utaratibu mzuri na ustaarabu wa maisha kwa wengine.

SOMA ZAIDI: Usemi ‘Mtoto kwa Mzazi Hakui’ Una Ukweli Kiasi Gani?

Mdau mmoja alitueleza hivi: “Nilivyo kuwa mtoto, mama yangu alinifundisha kuweka ganda la pipi, au karatasi, kwenye begi langu hadi nitakapoona pipa la taka, au kufika nyumbani. Mpaka leo, siwezi kamwe kutupa kitu barabarani. Imenibadilisha kabisa.”

Pia, tuwashirikishe kwenye shughuli za bustani. Hata tukiishi mjini, tunaweza kutumia chupa tupu, au ndoo chakavu, kupanda mboga ndogo kama mchicha, au sukuma wiki. Tukiwapa jukumu la kumwagilia mimea kila siku, wanajifunza kwamba uhai unahitaji uangalizi wa mazingira. 

Na mmea unaponyauka kwa sababu walisahau kumwagilia, au ikidhoofu na kudumaa kwa kuurundikia taka ngumu, wanajifunza moja kwa moja kutoka kwenye matokeo ya matendo yao kuwa kuyatunza mazingira ni kutunza na kujali maisha ya viumbe hai.

Tusisahau kuwa mazingira siyo ardhi pekee; ni maji, ni hewa, ni nishati pia. Tuwe na mazungumzo mepesi kuhusu matumizi ya umeme na maji. Tunapozima taa, au kufunga bomba la maji vizuri, tuwaambie kwa upendo: “Hii inasaidia dunia yetu kuwa salama.” Watoto wanapenda kuelewa “kwa nini,” na tunapowaeleza sababu, wanakuwa washirika wa kweli.

Hadithi nazo ni njia bora na rahisi ya mtoto kuelewa. Tuwasimulie hadithi za mti ulioota nje ya shule ukawa kivuli kwa watoto, au samaki aliyepoteza uhai kwa sababu ya plastiki. Tushiriki nao zoezi la  kupanda miti, kusafisha mtaa, au kuchora picha zinazoelimisha kuhusu mazingira. Kwa njia hii, wanaelewa si kwa nadharia tu, bali kwa hisia, uzoefu na vitendo.

SOMA ZAIDI: Tuanze Mazungumzo ya Fedha Nyumbani

Zaidi ya yote, tuwape nafasi ya kuongoza kwa njia zao. Wanaweza kubuni bango la mazingira kwa kalamu zao, kuanzisha kikundi shuleni cha kupanda miti, au hata kuandika shairi linalohimiza usafi. Tuwasikilize hata pale wanaposema kitu kinachoonekana kidogo kwa sababu ndani yake kuna mbegu ya mabadiliko makubwa.

Tukiwalea watoto wanaojali mazingira, tunawafundisha pia kuwa na huruma, kuwa na maono ya mbali, na kutenda kwa uadilifu. Ni kweli, dunia inakabiliwa na changamoto kubwa ya uharibifu wa mazingira, lakini pia tuna nafasi kubwa ya kujenga kizazi kinachojali zaidi, kinachofikiri kwa upana, na kinachotenda kwa hekima.

Tuanze leo tukiwa na imani kwamba mabadiliko ya kweli yanaanzia nyumbani.

Makala hizi za malezi huandaliwa na C-Sema, shirika lisilo la kiserikali linalojikita katika kuendeleza na kulinda haki za watoto Tanzania. Kwa maoni na ushauri, wapigie kwenye simu namba 116, ambayo ni maalumu kwa huduma za mtoto. Huduma hii haitozi malipo toka mitandao yote nchini. Vilevile, unaweza kuwapata kupitia kurasa za Facebook: Sema Tanzania, X: @SemaTanzania, na kupitia tovuti yao www.sematanzania.org.

Journalism in its raw form.

The Chanzo is supported by readers like you.

Support The Chanzo and get access to our amazing features.
Digital Freedom and Innovation Day
The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on Saturday April 20, 2024 at Makumbusho ya Taifa.

Register to secure your spot

Did you enjoy this article? Consider supporting us

The Chanzo is supported by readers like you.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Posts

×