Tanzania Yajitetea Umoja wa Mataifa Tuhuma za Kutesa, Kudhalilisha Wanaharakati, Yasema Inachunguza
Tanzania imejibu tuhuma zilizofikishwa katika Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa, juu ya kuwatesa na kuwafanyia udhalilishaji unaotweza utu wa binadamu, wanaharakati Agather Atuhaire kutoka Uganda na Boniface Mwangi kutoka Kenya, waliokamatwa mnamo Mei 19,2025 walivyokuja kuhudhuria kesi ya Tundu Lissu.
Akijibu hoja zilizowasilishwa na shirika la East and Horn of Africa Human Right Defenders Network, Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa, Balozi Abdallah Posi, alisema wanaharakati hao hawakusema sababu ya ukweli iliyowaleta Tanzania.
“Pamoja na kuwa shutuma zao dhidi ya serikali zina mashaka makubwa, tunayachukulia kwa uzito mkubwa madai ya kuteswa,unyanyasaji wa kingono na vitendo vya ukiukaji wa maadili. Ndio maana serikali kwa sasa inachunguza, na ikithibitika, wahusika watachukuliwa hatua,” alieleza Balozi Posi leo Juni 18, 2025.