Akizungumza na mawakili wa serikali leo, Julai 13, 2026,katika mkutano mkuu wa mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC). Rais Samia Suluhu ameeleza kuwa Tanzania ni bora kwenye kufuata haki za binadamu, huku akifafanua baadhi ya malalamiko ni hujuma kutokana na kasi ya ukuaji wa Tanzania.
“Kwa upande wetu sisi Tanzania, kwa muda mrefu tunaangalia haki za binadamu. Sasa haya yanayosemwa na mengine yatakayoendelea kusemwa, sisi tunajua jinsi tulivyo bora, lakini hata ulimwengu unajua,” ameeleza Rais Samia.
Rais Samia ameeleza kuwa baadhi ya mataifa yanaangalia njia ya kurudisha nyuma mataifa yanayoendelea na hoja haki za binadamu, ni moja ya jambo linaloibuliwa kwa mantiki hiyo.
“Jinsi nchi zetu hizi zinazoendelea, tunavyokwenda mbele, wengine wanaangalia njia na mbinu za kutuvuta nyuma ili tusiende kwa kasi ile ambayo tunakusudia,” anafafanua Rais Samia.
“Tunashuhudia mataifa yakihujumiana. Tunashuhudia vijana kulaghaiwa na kumezeshwa sumu dhidi ya mataifa yao na kushawishiwa kuhujumu chumi zao zilizojengwa kwa nguvu kubwa. Vilevile kuna wimbi la kuwaaminisha vijana kwamba serikali zao hasa za Afrika hazifuati au zinakiuka haki za binadamu,” aliendelea kufafanua.
Hotuba ya Rais Samia inakuja katika kipindi ambacho kumekuwa na shinikizo kutoka kwa wadau mbalimbali duniani, juu ya rekodi ya haki za binadamu ya Tanzania, huku matukio ya ukamataji, utekaji, kupotezwa kwa watu pamoja na mauaji ya Oktoba 29 yakitajwa.
Akifafanua zaidi Rais Samia ameeleza Haki za Binadamu zimewekwa katika Katiba na Sheria za Tanzania, na wananchi wakiwa na malalamiko wanaweza kwenda Mahakamani na kupata haki zao.
“Hata ulimwengu unajua sisi tuko wazuri [namna] gani au kiasi gani katika kuangalia haki za binadamu. Ila wanasema mpe mbwa jina baya ili ufanyaje, umuue,” aliendelea kueleza zaidi.
“Sisi Tanzania tuko vizuri kwenye haki za binadamu na uzuri ni kwamba hakuna aliye juu ya sheria zetu zilizowekwa. Hizo haki za binadamu zilizowekwa kwa sheria na sheria nyingine zozote, hakuna aliye juu ya sheria zetu. Anayevunja sheria atashughulikiwa,” alisisitiza.