The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on April 20, 2024. Register Here

Search
Close this search box.

Headlines

CHADEMA: Hatukubaliani na Kanuni za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa Zilizopitishwa
Habari Kubwa Leo Julai 16, 2024
Habari Kubwa Julai 15, 2024
Wafanyabiashara Kariakoo Waanza Mgomo
Habari Kubwa Leo Juni 18, 2024
Habari Kubwa Leo Juni 12, 2024
Habari Kubwa Leo Juni 11, 2024
Habari Kubwa Juni 5, 2024

Live Reporting

CHADEMA: Hatukubaliani na Kanuni za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa Zilizopitishwa

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimesema kuwa hakikubaliani na kanuni za uchaguzi wa Serikali za mitaa, vitongoji na vijiji, ambazo zimetolewa kupitia matangazo ya Serikali namba 571, 572, 573 na 574 ya tarehe Julai 12, 2024.

Kauli hiyo imetolewa leo Julai 19, 2024, na Katibu Mkuu wa chama hicho, John Mnyika, ambapo ameeleza kuwa msimamo wao huo umetokana na kitendo cha Wizara ya Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kupuuza mapendekezo ya CHADEMA kuhusu namna ambavyo kanuni hizo zingeweza kuboreshwa.

Mnyika ameeleza kwa kutokana na hali hiyo, kuna hatua mbili ambazo chama hicho kinahitaji kuzichukua kwa hivi sasa, moja ni kwenda mahakamani kuzipinga kanuni hizo na kuwe na utaratibu wa kisheria utakaowezesha uchaguzi wa haki kwa kusimamiwa na Tume Huru ya Uchaguzi.

Pili, kuendelea kujiandaa na mapambano na kuwatumia ujumbe wa wazi wezi wa uchaguzi kuwa umma hatutakuwa tayari ya 2019 yajirudie, kwani wanaona kwamba Rais Samia Suluhu Hassan hana nia ya kuendesha uchaguzi ambao utakuwa huru na wa haki. 

CHADEMA ilipata nafasi ya kutoa maoni yao kwa TAMISEMI kuhusu kanuni za uchaguzi huo Juni 15, 2024. Moja ya pendekezo lao ambalo halijazingatiwa ni kuhusu kuondolewa kwa mamlaka ya Waziri wa TAMISEMI kwenye uchaguzi huo.

Habari Kubwa Leo Julai 16, 2024

Utekelezaji finyu mapendekezo ya CAG yawaumiza vichwa wadau, watoa mapendekezo haya

Wadau mbalimbali wamemtaka Mdhibiti Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) aone umuhimu wa kuikutanisha ofisi yake, maafisa masuhuli, kamati za Bunge za usimamizi, kamati ya hesabu za Serikali Kuu, kamati ya Serikali za mtaa na kamati ya uwekezaji ili watafute suluhu ya utekelezaji finyu wa mapendekezo ya ripoti za CAG.

Wito huo umetolewa leo Julai 16, 2024, jijini Dodoma, wakati wa uzinduzi wa ripoti nne za uwajibikaji za taasisi ya Wajibu kwa mwaka 2022/2023, ripoti ambazo zimetokana na ripoti za CAG za mwaka 2022/2023.

Akizungumza kwenye uzinduzi huo Mkurugenzi wa taasisi ya Wajibu, Ludovick Utouh, amesema kuwa wito huo umetolewa kwa sababu kwa miaka mingi utekelezaji wa mapendekezo ya CAG haujawa wa kuridhisha. Mara nyingi hutekelezwa kwa asilimia 40, kwa hiyo asilimia 60 na zaidi yanabaki hajatekelezwa.

Taasisi ya Wajibu imekuwa ikitoa ripoti za uwajibikaji kila mwaka. Lengo likiwa ni kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu mambo muhimu yaliyoibuliwa  kwenye ripoti za CAG.

Wajibu huzisambaza ripoti hizo kwa wananchi lakini pia zinapatikana mtandaoni kwenye tovuti yao ya www.wajibu.or.tz

Tanzania na Oman zasaini maboresho ya mkataba wa usafiri wa anga

Tanzania na Oman zimesaini maboresho ya Mkataba wa Usafiri wa Anga (BASA) ili kuyawezesha mashirika ya ndege kutoka mataifa hayo kusafiri baina ya pande hizo bila kujali idadi ya safari au ukubwa wa ndege husika. 

Kusianiwa kwa mkataba huo kutayawazesha mashirika ya ndege yasiyokuwa na ndege pia kuungana na yale yanayomiliki ndege ili kuendesha biashara kwa pamoja. 

Hafla ya utiaji saini wa mkataba huo imefanyika leo Julai 15, 2024, na kushudiwa na Waziri wa Uchukuzi, Makame Mbarawa,  aliyeiwakilisha Tanzania na kwa upande wa Oman waliwakilishwa na Rais wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga wa nchi hiyo, Ali Nabri.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mbarawa amesema kuwa mkataba wa awali ulisainiwa mwaka 1982, hivyo maboresho yalikuwa ni muhimu. 

Mbarawa ameongeza kuwa mkataba huu wa sasa utafungua fursa mpya za usafiri baina ya nchi mbili hizi, kuleta ongezeko la abiria pamoja na kukuza biashara na uchumi.

Kwa upande wa Nabri amesema kuwa mkataba huo ni sehemu muhimu sana katika kuongeza ushirikiano kati ya Tanzania na Oman, lakini pia ni hatua muhimu katika kuboresha mazingira ya biashara na kukuza uchumi wa nchi zote mbili.

Tanzania, Marekani kushirikiana kupambana na ugonjwa wa saratani

Taasisi ya Biden Cancer Moonshot ya Marekani imeahidi kutoa ongezeko la kiasi cha dola za Kimarekani milioni 10 ambazo ni sawa na Shilingi za Kitanzania bilioni 300 kwa ajili ya kusaidia mapambano ya ugonjwa wa Saratani hususani katika nchi za Afrika.

Hayo yamebainishwa leo Julai 16, 2024, huko Washington DC, Marekani, wakati wa kikao kilichofanyika baina ya taasisi hiyo na Waziri wa Afya wa Tanzania, Ummy Mwalimu, aliyembatana Waziri wa Afya wa Zanzibar, Nassoro Mazrui.

Fedha hizo zinatarajiwa kuzisaidia nchi za Afrika kukabiliana na uhaba wa wataalamu, ukosefu wa miundombinu wezeshi, vifaa tiba hususani vya kutoa huduma za mionzi, takwimu, tafiti pamoja na ubunifu ili kuwezesha wananchi wake kupata huduma bora za saratani bila kikwazo.

Akizungumza kwenye kikao hicho Mwalimu amesema kuwa ugonjwa wa Saratani umekuwa ni changamoto kubwa nchini Tanzania ambapo inakadiriwa kuwa kuna ongezeko la wagonjwa wapya wa Saratani takribani 45,000 kila Mwaka.

Kwa upande wake mratibu wa taasisi hiyo, Catherine Young, wakati akifungua kikao hicho amesema kikao hicho muhimu kilikuwa ni kwa ajili ya kuwaleta pamoja wadau wakubwa wanaojishughulisha na ugonjwa wa Saratani ili kuwezesha nchi Afrika kupambana vyema na huo.

Habari Kubwa Julai 15, 2024

Serikali kukopa fedha NMB kwa ajili ya kununua mabasi 100 ya mwendokasi 

Msajili wa Hazina, Nehemia Mchechu, amesema kuwa Serikali imepanga kufanya mazungumzo na benki ya NMB kwa ajili ya kuona ni kwa namna gani wanaweza kupata fedha zitakazotumika kununua mabasi ya mwendokasi takribani 100 ili kukabiliana na upungufu mkubwa uliopo sasa. 

Mchechu ameyasema hayo leo Julai 15, 2024, jijini Dar es Salaam, wakati alipokuwa akizungumza na wahariri, ambapo ameeleza kuwa mabasi hayo ambayo wanategemea kuyapata ndani ya kipindi cha miezi sita toka watakapo toa oda hadi kuwasili, yatakuwa yakifanya kazi kwenye njia kuu peke yake. 

Akizungumzia kuhusu kampuni za usafirishaji kwenye mradi huo, Mchechu amesema kwamba ipo haja ya Serikali kuongeza idadi ya kampuni hizo ili zifanye kazi kwa ushindani na kuongeza ufanisi katika utoaji huduma.  

Mradi wa mwendokasi ulianza kufanya kazi mwaka 2016. Katika siku za hivi karibuni mradi huo umekuwa ukidaiwa kushindwa kuwahudumia ipasavyo wakazi wa jiji lenye watu wengi zaidi la Dar es Salaam, hali ambayo imekuwa ikipelekea usumbufu mkubwa. 

Mpaka mwezi Oktoba mwaka jana mradi huo ulikuwa una mabasi 210, lakini kati ya hayo, mabasi 140 pekee ndiyo yanayotoa huduma.

Wanaharakati waiburuza Serikali mahakamani kuzimwa kwa mtandao uchaguzi 2020

Mwanaharakati Kumbusho Dawson Kagine ameishtaki Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na Mwanasheria Mkuu kwa kitendo chao cha kuzima mtandao wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2020. 

Akizungumza na waandishi wa habari wakili anayesimamia kesi hiyo, Tito Mgoti, amesema kuwa kesi hiyo ni ya kikatiba na imefunguliwa katika Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Dar es Salaam kwa lengo la kuiomba mahakama iliangalie suala hilo kwa namna ambavyo Serikali ilikiuka haki za watu.

Magoti ameeleza kwamba mteja wake anadai tukio lile lilikiuka baadhi ya haki zake ambazo zimetajwa katiba, ikiwemo haki ya kupata, kutoa na kusambaza taarifa. Lakini vilevile, haki ya kujumuika na wengine, haki ya kushiriki katika masuala ya umma na vilevile Serikali imevunja wajibu wake kwa mujibu wa ibara ya 26 ambao ni wajibu wa kulinda na kutii na kuheshimu sheria za nchi.

Magoti ameongeza kuwa mteja wake anaitaka mahakama itamke kwamba tukio hilo halikuwa lakufaa, lilikuwa ni kinyume cha misingi ya utawala bora na lilivunja haki zake. Lakini pia, anaitaka Serikali ikiri kwamba haitarudia tena kufanya hivyo. 

Mashirika ya umma kuanza kuweka wazi taarifa zao za fedha 

Msajili wa Hazina, Nehemia Mchechu, leo Julai 15, 2024, ametangaza kuwa mashirika yote ya umma nchini yataanza kuchapisha wazi taarifa zao za kifedha ili kuhakikisha kunakuwa na uwazi na uwajibikaji kwenye mashirika hayo katika kipindi ambacho Serikali inaendelea kufanya mageuzi kwenye mashirika hayo.

Mchechu ameyasema hayo wakati alipokuwa akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari, kwenye kikao kilichofanyika hapa jijini Dar es Salaam, ambapo ameeleza kuwa kwa sasa taasisi za kifedha na kampuni zilizoorodheshwa kwenye soko la hisa pekee ndizo zinazotakiwa kuchapisha taarifa za kifedha. 

Hivyo, kwa sasa agizo hilo jipya litakwenda kwenye mashirika yote ambayo yanaendeshwa na Serikali. 

Mchechu akasisitiza kwamba umma lazima uarifiwe kuhusu utendaji wa kifedha wa taasisi zote za umma, ambapo uwazi huo utaweka wazi ni taasisi zipi zitalipa gawio kwa Serikali na zipi hazitafanya hivyo.

Wafanyabiashara Kariakoo Waanza Mgomo

Hali ya mitaa ya Kariakoo kwa siku ya leo Juni 24,2024, ni ya ukimya baada ya maduka katika eneo hilo muhimu la biashara kufungwa.

Maduka katika mitaa maarufu ya biashara na misongamano kama mtaa wa Congo, Msimbazi, Uhuru yote yalikuwa yamefungwa.

Katika baadhi ya maeneo matangazo yameonekana yenye kichwa, Kufunga Biashara Zetu, “Tangazo kuanzia leo 24/6/2024 tunafunga maduka yetu kwa muda usiojulikana mpaka Bunge litakapo ondoa sheria kandamizi zinazopora mitaji ya wafanyabiashara,” ilisoma sehemu ya tangazo hilo.

Vipeperushi juu ya mgomo huu vilianza kusambaa wiki iliyopita, huku viongozi wa wafanyabiashara hao wakionesha kuwa havikutoka kwao.

Polisi na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam wametoa onyo kwa wafanyabiashara hao.

Habari Kubwa Leo Juni 18, 2024

Wadau walaani mauji ya mtoto mwenye ualbino 

Wadau mbalimbali nchini wakiongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan, leo Juni 18 2024, wamejitokeza hadharani kulaani na kukemea vikali mauaji ya mtoto mwenye ualbino, Asimwe Novath, ambaye alitekwa na watu wasiojulikana Mei 30, 2024, wakati akiwa nyumbani kwao na mwili wake ukapatikana jana Juni 17, 2024, ukiwa hauna baadhi ya viungo.  

Akizungumza kwa uchungu bungeni kuhusu tukio hilo ambalo limetokea wilaya ya Muleba, mkoani Kagera, mbunge wa viti maalumu kupitia Chama cha Mapinduzi anayewakilisha watu wenye ulemavu, Khadija Shaaban maarufu kama Keisha, ameiomba Serikali itunge sheria kali zitakazokomesha mauaji hayo. 

Khadija ameongeza kuwa watu wenye ualbino hawana amani na wanaamini kuwa katika kipindi hiki cha uchaguzi kinaweka maisha yao hatarini kutokana na uwepo wa imani hasi zilizojengwa kwa watu wenye ulbino.  

Matukio ya watu wenye ualbino kushambuliwa au kutekwa katika kipindi cha hivi karibuni yalipungua, na mwaka 2023 haikuripotiwa kabisa.

Licha ya hali kuonekana shwari, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kupitia ripoti yake ya mwaka 2023 kilitoa angalizo la kuwepo kwa hofu baina ya watu wenye ualbino kwenye baadhi ya maeneo.

Tanzania yaanza kujenga majengo ya kitega uchumi nje ya nchi 

Tanzania imeanza kutekeleza mpango wake wa kujenga majengo ya kitega uchumi kwenye mataifa mbalimbali kwa kuzindua ujenzi wa majengo pacha yenye ghorofa 22 kila moja huko Upper Hill, katikati mwa jiji la Nairobi, majengo ambayo pia yatakuwa ni makazi ya ubalozi wa Tanzania nchini humo.

Akizungumza kuhusu mpango huo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, January Makamba, amesema awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mpango huo itahusisha majiji ya Nairobi, Kigali, Kinshasa, London, New York na Lusaka ambapo Serikali itapata takribani Shilingi bilioni 36 kwa mwaka kutokana na uwekezaji huo.

Makamba ameongeza kuwa kwa sasa Serikali inatumia takriban Shilingi bilioni 29 kwa mwaka kwa ajili kukodisha ofisi za ubalozi na nyumba za watumishi wa ubalozi kitu ambacho mpango huo utakwenda kikutatua. 

Kwa sasa Serikali ya Tanzania inamiliki takriban majengo na viwanja 101 duniani kote ambapo vingi vipo katika maeneo ya miji mikuu. Katika jiji la Lusaka pekee Serikali inamiliki majengo na viwanja 11. 

Spika Tulia Ackson ataka Mpina ahojiwe na Kamati ya Haki na Maadili

Spika wa Bunge, Tulia Ackson, leo Juni 18, 2024, ametoa maelekezo kwa Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge imuhoji mbunge wa Kisesa kupitia Chama cha Mapinduzi,  Luhaga Mpina, kwa madai ya utovu wa nidhamu ikiwemo kudharau mamlaka ya Spika na kumkabidhi taarifa yao Juni 24, 2024.  

Kauli hii ya Spika inatokana na Mpina kumtuhumu Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe, kuwa alilidanganya Bunge kuhusu vibali vya kuagiza sukari na hivyo kutakiwa kuwasilisha ushahidi wake mbele ya Spika.

Spika amesema licha ya Mpina kuwasilisha ushahidi huo, kabla ya hatua kuchukuliwa ikiwa ni pamoja na Kamati ya Bunge kuifanyia uchunguzi, Mpina aliwasilisha madai hayo kwenye vyombo vya habari, kitendo ambacho kimeelezwa kuwa ni kinyume na kanuni za Bunge.

Juni 4, 2024, wakati wa mjadala wa hoja ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha kwa mwaka fedha 2024/2025, Bashe alisema kwamba kampuni na viwanda vya sukari vilivyopewa dhamana na Serikali ya kuhakikisha kunakuwa na sukari ya kutosha vimeshindwa kutekeleza wajibu huo kwa kushindwa kuagiza bidhaa hiyo, hali ambayo ilisababisha uhaba wa sukari nchini.

Habari Kubwa Leo Juni 12, 2024

ACT Wazalendo, CHADEMA waishutumu TAMISEMI kwa kupoka majukumu ya Tume ya Uchaguzi 

Vyama vya upinzani vya ACT Wazalendo na  CHADEMA vimeishutumu Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kuwa haistahili kusimamia zoezi la uchaguzi wa Serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika baadaye mwaka huu, kwani kwa kufanya hivyo itakuwa inapoka mamlaka ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC). 

Kauli hiyo imetolewa kufuatia wizara hiyo kuvitaarifu vyama hivyo kuwa vinaalikwa kutoa maoni kuhusu rasimu ya kanuni za uchaguzi wa Serikali za mitaa wa mwaka 2024, zoezi ambalo limeelezwa kuwa litafanyika Juni 15, 2024, jijini Dodoma. 

Madai haya yanatokana na kile kilichoelezwa kwenye Sheria ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi ya mwaka 2024,  kifungu cha 10 (1) (c ), kuwa tume hiyo ndiyo itakuwa na wajibu wa kusimamia na kuratibu uendeshaji wa uchaguzi huo lakini kwa utaratibu utakaoainishwa na sheria itakayotungwa na Bunge. 

Hata hivyo, tangu sheria hiyo ilivyopitishwa Aprili 2024 hakujawa na mchakato wowote wa kupelekwa kwa muswada bungeni ili sheria itakayosimamia uchaguzi huo iweze kutungwa. 

Reli ya TAZARA kufumuliwa kwa ajili ya marekebisho 

Serikali za Tanzania, Zambia na China zipo katika hatua za mwisho za mazungumzo ya mpango wa kuifumua reli ya TAZARA kwa ajili ya kuiboresha na kuimarisha shughuli za usafirishaji. 

Hayo yamebainishwa na leo Juni 12, 2024, bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, wakati akijibu swali mbunge wa Mlimba kupitia Chama cha Mapinduzi, Godwin Kunambi, aliyehoji mkakati wa Serikali kuboresha miundombinu ya reli hiyo inayounganisha nchi ya Tanzania na Zambia. 

Kihenzile ameongeza kuwa mpaka sasa tayari kikao kimeshafanyika kati ya Rais wa Tanzania, China na Zambia kwa ajili ya kufumua, na kukarabati reli hiyo lengo likiwa ni kuongeza uwezo wa kubeba mizigo, kuongeza vichwa vya treni pamoja na mabehewa ya kubebea mizigo ya abiria.

Reli ya TAZARA yenye urefu wa kilomita 1,860 ilijengwa kwa ushirikiano wa mataifa ya Tanzania, Zambia na China na ikaanza kufanya kazi rasmi Julai 14, 1976. Reli hiyo imekuwa kiungo kikubwa cha biashara baina ya Tanzania na Zambia kwani imekuwa ikisafirisha mizigo na raia baina ya mataifa hayo. 

Wizara ya Madini yazindua timu yake ya kuandaa andiko la maudhui ya utafiti wa madini

Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, leo Juni 12, 2024, amezindua timu itakayokwenda kuandika andiko la maudhui ya utafiti wa madini lililopewa jina la ‘vision’ 2030, andiko ambalo linatarajiwa kutoa dira ya kufikia asilimia 50 ya utafiti wa madini ifikapo mwaka 2030.   

Akizungumza katika uzinduzi huo ambao umefanyika jijini Dodoma, Mavunde amesema kuwa utafiti wa madini uliofanyika kwa nchi nzima hadi hivi sasa upo kwa asilimia 16 tu, ndiyo maana wakaona haja ya kuunda timu hiyo ili itoe taswira mpya ya sekta hiyo muhimu. 

Waziri huyo ametangza kuwa timu hiyo itaongozwa na Profesa Abdulkarim Mruma ndani yake ikiwa na wajumbe wengine 12 ambao watatakiwa kuzifanyia kazi hadidu za rejea 14 walizopewa. 

Nchini Tanzania, sekta ya madini ni moja ya sekta zinazochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya wananchi. Kwa mfano, kwa mwaka wa fedha uliopita wa 2022/2023, migodi ilifanya manunuzi ya dola za Kimarekani bilioni 1.6, ambapo dola bilioni 1.4 zilihusisha kampuni za Kitanzania na hivyo kufanya zaidi ya asilimia 86 ya manunuzi yote ya migodi katika mwaka huo yawe yamefanywa na Watanzania.