Mchungaji Awekwa Kizuizini Zanzibar Kisa Jina Linaonekana la Kiislam

Mustafa Abubakar alizaliwa Muislam kabla ya kubadili dini na kuwa Mkristo lakini bila ya kubadilisha jina alilopewa na baba yake.

subscribe to our newsletter!

Dar es Salaam. Maafisa Uhamiaji visiwani Zanzibar wameshukiwa kumuweka kizuizini mchungaji wa dini ya Kikristo aliyekuwa amekwenda visiwani humo kwa ajili ya kukutana na makundi mbalimbali ya Wakristo, wakiwemo baadhi ya wanafunzi wa vyuo vikuu wa Kikristo, kueneza kile mchungaji huyo amesema ni “neno la Mungu.”

Mustafa Abubakar aliwekwa kizuizini mnamo Septemba 11, 2021, katika Bandari ya Zanzibar baada tu ya kushuka boti iliyokuwa ikitokea Dar es Salaam baada ya maofisa wa uhamiaji kumtilia shaka kwamba siyo mchungaji kwa kuwa hati yake ya kusafiria ilibeba jina ambalo wao Uhamiaji wanaamini ni la Kiislamu – Mustafa Abubakar.

The Chanzo haikuweza kumpata mara moja Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar Masoud Sururu kusema kama anafahamu kama tukio hili lilitokea.

Akisimulia mkasa huo kwa shirika lisilo la kiserikali linalojihusisha na kuwatetea Wakiristo wanaonyanyaswa duniani la International Christian Concern (ICC), Abubakar, ambaye alizaliwa na kukulia kwenye familia ya Kiislamu huko Mombasa, Kenya kabla ya kuamua kubadilisha dini na kuwa Mkristo, anasema Uhamiaji walikataa kumuamini licha ya kutumia juhudi kubwa za kuwashawishi.

“Afisa aliyekuwa ameshikilia hati yangu ya kusafiria akamwita mkuu wake na wakaniweka ndani ya chumba kidogo pale pale bandarini [Zanzibar],” Abubakar anasimulia. “Walinihoji kwa zamu, ikiwemo hata kuwapigia maofisa wengine kuniuliza maswali ya ninakotoka na nimekuja [Zanzibar] kufanya nini. Niliwaambia mimi ni Mkristo na jina langu ni Mustafa Abubakar kwa sababu hilo ndo jina nimepewa na baba yangu. Walinitisha kwamba nisipowaambia ukweli, watanikatalia kuingia Zanzibar na kunirudisha Dar es Salaam.”

Baada ya masaa kama mawili kupita huku Uhamiaji wakionekana kutoshawishika na maelezo ya Abubakar, maofisa hao walimpatia mchungaji huyo fomu ya kujaza ili wamrudishe Dar es Salaam bila ya kuingia Zanzibar.

“Wakati nikiwa najaza hiyo fomu, mwenyeji wangu alipiga simu akiniuliza mbona nilikuwa nachelewa kufika,” Abubakar anasimulia. “Maofisa wa Uhamiaji wakaniambia niiweke simu kwenye loudspeaker au vinginevyo wangenipokonya. Nilitii. Mwenyeji wangu akamsifu Bwana [Yesu Kristo] kwamba nimefika salama [Zanzibar] na kunitaka niharakishe kwani baadhi ya waumini walishakusanyika kunisubiria. Hapo ndipo maofisi wale walipoamini kwamba nilikuwa naongea ukweli.”

Abubakar alifanikiwa Zanzibar, huku akidai kwamba maofisa wa Uhamiaji walimpa sharti la kutokuongea kwenye mikutano mikubwa au mihadhara, wakisema kwamba akifanya hivyo anaweza kukamatwa na kushtakiwa.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Posts