The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on April 20, 2024. Register Here

Search
Close this search box.

TAWA Yadaiwa Kushikilia Trekta za Wakulima Kilombero

Mamlaka hiyo ya uhifadhi wa wanyamapori yadai wakulima hao walivamia eneo la hifadhi, madai ambayo wakulima na mamalaka nyengine za Serikali zinapingana nayo.

subscribe to our newsletter!

Morogoro. Mamlaka ya Uhifadhi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) inashikilia trekta na zana nyingine za kilimo walizo zichukua kutoka kwa wakulima kutoka kijiji cha Msita, kata ya Chita, wilayani Kilombero, mkoani Morogoro tangu Novemba 2021 baada ya kuwatuhumu kwamba wamevamia eneo la hifadhi.

Hilo liligundulika hivi karibuni kufuatia hatua ya wakulima hao kulalamikia kunyang’anywa huko kwa vitendea kazi vyao hivyo muhimu wakati wa mahojiano na redio ya MVIWATA FM inayomilikiwa na Mtandao wa Vikundi vya Wakulima Tanzania (MVIWATA) yaliyofanyika Januari 30, 2022.

“Mnamo Novemba 2021, walitukamata watu wa hifadhi wakidai eneo tunalolima ni eneo lao,” alisema Mohamed Ally, mmoja kati ya wakulima ambao trekta zao zilikamatwa. “Tulirudi ofisi ya kijiji ambao walisema eneo [tulilolima] siyo eneo la hifadhi, hivyo polisi.” 

Licha ya kwamba Serikali ya kijiji ilibainisha kwamba eneo walilokuwa wakilima wakulima hao ni sahihi na hakukua na uvamizi wowote, TAWA bado inaendelea kushikilia vitendea kazi vya wakulima hao, hali wanayosema inaathiri sana maisha yao ya kila siku.

“Tunaomba Serikali itusaidie kwani mbali na juhudi zote hizo bado wameshikilia trekta ambayo nimenunua kwa mkopo ili niweze kufanya kazi na kurudisha mkopo,” alisema Ally.

Mnamo Februari 4, 2022, Msimamizi wa TAWA Lawrence Okode amekiri kukamatwa kwa trekta hizo huku akisisitiza kwamba hatua hiyo ilikuwa ni sahihi kwa wakulima hao walivamia eneo la hifadhi.

”Kwa haraka haraka ninachoweza kukwambia ni kwamba, hifadhi ipo inaitwa Pori Tengefu Kilombero,” Okedo aliiambia MVIWATA FM kwa njia ya simu iliyomtafuta kujibu shutuma hizo. 

“Bikoni zipo tuliziweka tangu 2017,” aliongeza. “Na humo ndani tulipoweka bikoni haruhusiwi mtu kulima. Hatakiwi mtu kuua mnyama pori. Hatakiwi mtu kuchunga ng’ombe humo ndani na shughuli za kibinadamu kama uvuvi haramu. Kuna uvuvi ambao unaruhusiwa ambao unaratibiwa na TAWA.”

Malalamiko ya wakulima hawa kwa sasa yapo mikononi mwa mwa Mkuu wa Wilaya ya Kilombero Hanji Godigodi ambaye ameahidi kuyafanyia kazi ambapo tayari ametuma timu yake huku akiwataka wananchi hao wa kijiji cha Msita kuendelea na shughuli zao za kilimo.

“[Hawa] wakulima [ambao trekta zao zimekamatwa] walikuwa nyuma ya eneo ambalo mtu amejenga, anaishi na kufuga kuelekea uelekeo wa hifadhi,” MVIWATA FM ilimnukuu Godigodi akizungumza. “Lakini yeye hakukamatwa, kwamba hayuko eneo la hifadhi. Sasa iweje huyu wa nyuma anakamatwa na anakibali cha kijiji? Okode nilimuuliza lakini hakunipa majibu ya kuridhisha. Hivyo, nasubiri hiyo taarifa ya OCS ndiyo inaweza kutupa mwelekeo.”

Halmashauri ya wilaya ya Kilombero imekuwa ikikumbwa na migogoro mingi ya ardhi kati ya wakulima na mamlaka mbalimbali za Serikali pamoja na wawekezaji na wafugaji.

Digital Freedom and Innovation Day
The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on Saturday April 20, 2024 at Makumbusho ya Taifa.

Register to secure your spot

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *