The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on April 20, 2024. Register Here

Search
Close this search box.

Wananchi Ngorongoro Hatarini Kukosa Huduma Serikali Ikihamishia Miradi Handeni

Hatua hiyo inakuja takriban mwezi mmoja tangu Serikali itangaze kutengwa kwa eneo maalum wilayani Handeni kwa ajili ya wananchi wa Ngorongoro watakaokuwa tayari kuhama kutoka kwenye hifadhi ya Ngorongoro kwa hiari.

subscribe to our newsletter!

Dar es Salaam. Serikali inakusudia kuhamisha fedha za miradi ya UVIKO-19 kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro kwenda Halmashauri ya Wilaya ya Handeni katika uamuzi ambao umekosolewa na wanaharakati wa haki za binadamu wanaodai uamuzi huo unalenga kuwaadhibu wananchi wa Ngorongoro ambao mpaka sasa wamegoma kuhama kwenye ardhi yao hiyo ya asili.

Uamuzi huo umedhihirika baada ya kuvuja kwa barua mbili za Machi 31, 2022, kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Ngorongoro kwenda kwa Walimu Wakuu wa shule za sita za msingi na sekondari zikiwaelekeza wakuu hao wa shule kuhamisha fedha walizopewa kutoka kwenye mradi wa UVIKO-19 kwenda Wilaya ya Handeni.

Kwa mujibu wa barua ya kwanza, yenye kumbukumbu namba NGOR/DC/F.1/02/VOLIII/68, na kusainiwa na Dk Jumaa Mhina, Walimu Wakuu wa Shule za msingi za Endulen, Misigyo na Essere wanapaswa kuhamisha jumla ya Sh160,000,000 kwenda Wilaya ya Handeni: Endulen Sh80,000,000; Misigyo Sh40,000,000; na Essere Sh40,000,000.

Barua nyengine yenye kumbukumbu namba NGOR/DC/F.1/02/VOLIII/69 imepelekwa wa Wakuu wa Shule za Sekondari za Embaraway, Nainokanoka, na Shule ya Wasichana Ngorongoro ambazo kwa pamoja zinapaswa kurejesha jumla ya Sh195,500,000: Embaraway Sh66,000,000; Nainokanoka Sh80,000,000; na Shule ya Wasichana Ngorongoro Sh49,000,000.

Fedha hizo zilitolewa na Serikali ikiwa ni sehemu ya Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO -19. Tanzania imepanga kutumia jumla ya Shilingi trioni 1.3 kukabiliana na athari zitokanazo na janga la UVIKO-19. Fedha hizo ni mkopo kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF).

Barua hizo zilizopelekwa kwa Wakuu wa shule husina na ambazo zinaendelea kuzunguka mitandaoni hazisemi kwa nini shule hizo zinapaswa kuhamishia fedha hizo wilayani Handeni.

Hata hivyo, barua hizo zimeibuka takriban mwezi mmoja tangu Serikali itangaze kwamba imetenga eneo maalum wilayani Handeni kwa ajili ya wananchi wa Ngorongoro watakaokuwa tayari kuhama kutoka kwenye hifadhi hiyo ambayo Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) linaitambua kama moja ya urithi wa dunia.

Serikali imepanga kuwahamisha Wamaasai wapatao 70,000 kutoka Ngorongoro kufuatia madai kwamba hifadhi hiyo ipo katika hatari ya kupotea kutokana na shughuli za binadamu ikiwemo mifugo.

Mnamo Machi 11, 2022, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alisema tayari amepokea orodha ya kaya za awali 86 zenye watu wapato 453 ambao wamekubali kuondoka “kwa hiari yao” kwenye Hifadhi ya Ngorongoro huku wengine wakiendelea kujiandikisha, taarifa ambayo ilipingwa vikali na wawakilishi wa wananchi waioshio Ngorongoro pamoja na wanaharakati wa haki za binadamu.

Akizungumzia hatua hiyo ya kuhamisha fedha kutoka Ngorongoro kwenda Handeni, Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC) Onesmo Olengurumwa amesema uamuzi huo unahuzunisha sana lakini hana cha kusema kwa sasa ila anajua Mungu anaona.

“Hivi ndivyo watu wangu wa Ngorongoro wanavyofanyiwa,” alisema Olengurumwa, ambaye asili yake ni Ngorongoro, kwenye mtandao wa Twitter akiambatanisha barua husika. “Sijui tumewakosea nini Ngorongoro. Naendelea kutafakari nini cha kufanya.”

Digital Freedom and Innovation Day
The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on Saturday April 20, 2024 at Makumbusho ya Taifa.

Register to secure your spot

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *