Serikali imetoa taarifa kukanusha kuwa kuna mgongano au kuvunjwa kwa Mkataba wa uanzishwaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kufuatia Angela Kizigha, Dkt. Ngwaru Maghembe na James Milya kuwa wabunge wa Bunge la Tanzania kupitia kuchaguliwa na kuteuliwa.
Wadau mbalimbali ikiwemo Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu wamekuwa wakihoji uhalali wa Wabunge hao kuendelea kuwa Wabunge wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki ilhali Mkataba umeweka sharti kuwa wabunge wa nchi husika hawatakiwi kuwa wawakilishi katika chombo hicho.
Katika tamko lake la Aprili 09, 2026, LHRC iliitaka Serikali kutoa ufafanuzi wa kina kuhusu uhalali wa Wabunge hao katika Bunge la Afrika Mashariki.
Katika ufafanuzi uliotolewa na Msemaji wa serikali, Gerson Msingwa, leo Aprili 10, 2026, amesisitiza kuwa watatu hao sio Wabunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA).
“Kwa mujibu wa Ibara ya 51(3) (c) ya Mkataba wa Kuanzishwa kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mbunge wa EALA hukoma kuwa Mbunge endapo atateuliwa kuwa Mbunge wa Bunge la nchi mwanachama,” Msigwa ameeleza katika taarifa yake.
“Kutokana na masharti hayo, ubunge wa EALA kwa Mheshimiwa Angela Kizigha na Waheshimiwa Dkt. Ngwaru Maghembe na James Milya ulikoma baada ya kuteuliwa-kuchaguliwa kuwa wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” taarifa hiyo iliongeza.
Serikali imeeleza kuwa Bunge litajaza nafasi hizo kwa mujibu kanuni na taratibu ikiwemo mchakato kuanzia katika vyama vya siasa.
Jesca Samwel John ni mwandishi wa The Chanzo Dar es Salaam