The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on April 20, 2024. Register Here

Siku ya Tatu ya Kesi ya Kikatiba Juu ya Haki ya Faragha na Mawakili: Lissu Amhoji Mkuu wa Gereza, Majaji Wauliza Viongozi wa CHADEMA Kuzuiliwa Kumtembelea

Lissu amehoji juu ya mawakili wake na viongozi wenzake wa CHADEMA kuwekewa vikwazo kumuona, hoja ambazo Mkuu wa Gereza amezikanusha

subscribe to our newsletter!

Dar es Salaam-Shauri la Kikatiba lililofunguliwa na mawakili wa Tundu Lissu, juu ya kunyimwa haki ya faragha na mteja wao limeendelea Julai 22, 2026, ikiwa ni siku ya tatu ya shauri hili. Tundu Lissu amemhoji Mkuu wa Gereza la Ukonga, Andrew Shabani Ntamamiro. Sehemu kubwa ya mahojiano ni juu ya taratibu anazozi simamia  ikiwemo kuruhusu au kutoruhusu baadhi ya watu kumtembelea Tundu Lissu.

Shauri hilo la kikatiba namba 7300/2026 limefunguliwa na mawakili William Maduhu, Nashon Nkung na Paul Kisabo ambapo linasikilizwa mbele  ya jopo la majaji watatu Amir Mruma ambaye ni mwenyekiti wa jopo hilo, Dkt. Angelo Rumisha na Dkt. Evaristo Longopa. Wajibu maombi katika shauri hili wako wanne, ambapo wa kwanza ni Mwanasheria Mkuu, wa pili ni Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, wa tatu ni Mkuu wa Gereza Ukonga, wa nne ni Tundu Lissu na wa tano ni Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS).

Mahojiano kati ya Lissu na Mkuu wa Magereza Ukonga yalianza kwa Lissu kuhoji juu ya misingi ya kisheria ya utendaji wa Maofisa wa Magereza ambapo Lissu alianza kuhoji juu ya kanuni zinazotumika kuamua taratibu za Magereza, ambapo kupitia Kifungu cha 105 cha Sheria ya Magereza alionesha mwenye Mamlaka ya kutunga kanuni ni Waziri na pia kupitia kifungu cha 5 cha sheria hiyo hiyo Lissu alionesha Kamishna wa Magereza anaweza kuamua taratibu mbalimbali kwa muongozo wa kanuni zinazoundwa na Waziri.

SOMA: Siku ya Pili ya Kesi ya Kikatiba ya Lissu Juu ya Haki ya Faragha na Mawakili: Ahoji Utaratibu wa Wafungwa Waliohukumiwa Kifo Kutumika Dhidi Yake

Baada ya Lissu kuonesha msingi wa utaratibu wa Magereza huwekwa kikanuni, akaendelea kuhoji juu ya matukio na uzoefu wake wa moja kwa moja.

Lissu: Kwa kanuni hizo wafungwa wamegawanywa kwa makundi matatu? Au unataka nikutajie?

Ntamamiro: Nitajie

Lissu: Wapo watoto, wapo wafungwa wanaoitwa star prisoners, na kundi la tatu ni wafungwa wa kawaida?

Ntamamiro: Ni kweli kabisa.

Mhe. Lissu: Hao wanaoitwa young prisoners ni wenye chini ya miaka 21.

Ntamamiro : Ni kweli

Mhe. Lissu: Wanaoitwa wafungwa nyota ni wale first offenders? Wamefanya kosa kwa mara ya kwanza?

Ntamamiro : Kweli

Lissu: Oridinary ni wale wafungwa wengine wanaobaki wote wasio kundi la kwanza na la pili?

Ntamamiro : Ni kweli.

Lissu: Jana ulimsikia Kalokola wakili wa serikali akisema kuna wafungwa wa umuhimu wa kisiasa au alisema  Prisoners of Security Importance, je kwa kanuni hizo wapo?

Lissu aliendelea kumuuliza shahidi kama Mkuu yeyote wa gereza au Kamishna wa Magereza ana uwezo wa kubadili kanuni, ikiwemo kubadili makundi ya wafungwa ambapo Ntamiro alijibu kuwa hakuna mwenye mamlaka ya kufanya hivyo.

Sehemu kubwa ya mahojiano ya Lissu amekuwa akijaribu kuonesha namna ambavyo kanuni hazifuatwi katika uzoefu wake Magerezani, huku Mawakili wa serikali wakijaribu kuonesha kanuni zinafuatwa. Akimhoji shahidi, Lissu alianza kwa kuufungua zaidi ushahidi uliotolewa na Mawakili wake kwa kutaja majina ya maofisa mbalimbali, akiwahusisha na kuhudhuria na kusikiliza alipokutana na mawakili wake.

Katika ushahidi wa mawakili wa Lissu walieleza kuwa maeneo wanayokutana na Lissu huwa hayana faragha na Maofisa wa Magereza husikiliza kila kitu, ikiwemo kunakili kumbukumbu.

Lissu: Shahidi tuambie Mkuu wa Gereza la Ukonga una matatizo ya kusikia au hauna?

Ntamamiro: Niko vizuri mimi. Nasikia.

Mhe.Lissu: Assistant Commisioner of Prison, Recha. Ana matatizo ya kuona na kusikia au hana?

Ntamamiro : Sijui.

Lissu: Je ACP Mumbii nae ana matatizo ya kusikia?

Ntamamiro : Mimi sio Daktari sijui.

Lissu: Je ACP Mohamed nae?

Ntamamiro : Nae pia sijui kama ana matatizo ya kusikia.

Lissu: SGT. Hamisi vipi nae anasikia au hasikii?

Ntamamiro: Sijui.

Lissu : Inspector  Stima legal officer nae vipi anasikia?

Ntamamiro: Nae pia sijui.

Mhe. Lissu: Wale akina mama watatu wanaofanya kazi admission office wana matatizo ya kusikia na kuona au hawana?

Ntamamiro : Sijui.

Lissu: Koplo Dani mtunza fedha nae vipi ana matatizo ya kusikia au vipi? Maana na yeye mara zote huwa yuko ofisi ya admission?

Ntamamiro: Sijui.

Lissu: Wale maaskari ambao huwa wanatoka na mimi ninakolala na kunileta kwako Insp. Kaisi na Mwingia nao pia huwa wanatatizo la kusikia?

Ntamamiro : Sijui.

Lissu: Je kwa uzoefu wako Jeshi la Magereza linaweza kuajiri askari haoni au hasikii?

Ntamamiro : Haliwezi kuajiri. Lakini unaweza kuumwa ukiwa kazini.

Lissu: Akiajiriwa akapofuka ataendelea kuwa Askari Magereza.

Ntamamiro: Mimi sio daktari

 Lissu: Kama atakuwa hasikii je ataendelea kuwa askari magereza?

Ntamamiro : Sina jibu.

Lissu: Hata kutokuwa na jibu ni jibu pia.

Lissu akionesha chakula chake wakati wa mapumziko ya kula

Katika maswali aliyoyajibu Ntamamiro aliweza kuonesha kuwa alianza kazi katika gereza la Ukonga mnamo Septemba 2025, hii ni baada ya kupata uhamisho. Ubishani wa hoja ulitokea kati ya Lissu na Ntamamiro pale alipokataa juu ya uwepo wa maofisa wake katika mazungumzo mbalimbali ya Lissu na mawakili, ambapo Lissu  aliweza kumpitisha mkuu huyo wa gereza katika nyaraka mbalimbali akijaribu kuonesha matobo katika maelezo ya shahidi huyo.

Lissu: Waeleze majaji kama kuna sharti lolote la kisheria kwamba mfungwa yeyote mwenye wakili aa mawakili anapaswa kuwasilisha orodha ya mawakili wake kwa Bwana Jela?

Ntamamiro : Halipo kisheria. Lakini mfungwa ana haki ya kuchagua nani amtembelee.

Lissu: Nilichagua kuwa Kulwa William Maduhu na umemkatalia?

Ntamamiro  : Hakuwepo kwenye orodha.

Lissu: Andrea Chima alikuja kuniona yupo kwenye orodha gani?

Ntamamiro : Hayupo.

Lissu: SUPP 5 twende sasa tarehe 24/12/2025 angalia kwenye entry kuna Nashon Nkungu na Paul Kisabo?

Lissu: Mazungumzo na Nashon ulisema asimamiwe kwa Makamu mkuu wa gereza na kuwataka wasaidizi wako wanne wasimamie? Na mazungumzo ya Kisabo pia ulisema yasimamiwe kwenye ofisi ya Kaimu Mkuu wa Gereza.

Ntamamiro : Ndio

Lissu: Na tunakubaliana wale watu wote akina Mumbii, legal officer Stima, Koplo Dani, na akina mama watatu. Je hawa watu wanakuwemo humo?

Ntamamiro : Si kweli. Huwa wanatoka. Wanaacha mazungumzo yafanyike.

Jaji: Lissu umeridhika na majibu ya shahidi.

Lissu: Ngoja nataka kukamata watu waongo.

Lissu: Kumbe maafisa wote mle chumbani wanatoka nje, sasa soma kiapo chenu ndugu yangu. Nakusomea kwenye kiapo chako. Kiapo kinasomeka kuwa walikuwepo.

Ntamamiro: Kuna ambao walikuwepo na kuna ambao walitoka.

Mhe. Lissu: Waliokuwepo ni akina nani?

Ntamamiro: Waliosindikiza

Mhe. Lissu: Akina nani?

Ntamamiro : Sikumbuki

Katika ushahidi wake Ntamamiro alipinga baadhi ya hoja zilizotolewa na Lissu na Mawakili wake  ikiwemo uwepo wa CCTV kwenye chumba cha mawasiliano ya simu aliyokuwa akitumia kuongea na mawakili wake kwenye kioo, na pia alipinga kuwa kuna Askari wanaosikiliza simu hizo kwenye chumba maalum.

Lissu alitumia muda kuhoji juu ya kuzuiwa kwa viongozi na CHADEMA kuweza kumtembelea na kuzungumza naye, jambo lililofanya katikati ya mahojiano, Mwenyekiti wa Jopo la Majaji kuhoji juu ya utaratibu huo, huku Mkuu wa Gereza Ukonga akiishia kuomba radhi.

Lissu: Je ni kweli kwamba baada ya matukio ya Oktoba 29 uliniita ofisini kwako?

Ntamamiro: Sio kweli

Lissu:Ulivyoniita ukaniambia kuanzia sasa ni marufuku viongozi wa CHADEMA na wanachama kuja kukutembelea.

Ntamamiro : Sio kweli

Lissu: Na ukasema mazungumzo yako na mawakili yatakuwa kwa mambo ya kisheria tu?

Ntamamiro : Sio kweli.

Lissu: Wakili Gaston Garubindi alikuwa anakuja kunitembelea Gerezani kabla ya tarehe 14/11/2025

Ntamamiro: Kweli

Lissu: Kuanzia hiyo tarehe hajawahi kuruhusiwa?

Ntamamiro: Simpangii.

Lissu: Kuanzia niingie Gerezani Wakili Dickson Matata na Deogratias Mahinyila hujawahi kuwaruhusu waingie gerezani. Huyu Matata ni Mwenyekiti Kanda ya Magharibi na Mahinyila ni Mwenyekiti wa Vijana Taifa hawajawahi kuruhusiwa?

Ntamamiro: Siwalazimishi waje au wasije.

Lissu: Kumbe ndio hivyo. Haya Mahinyila na Matata kesho njooni Ukonga.

Ntamamiro: Kesi iko Mahakamani sitawaruhusu

Mhe. Lissu: John Heche, Amani Golugwa, Katibu Mkuu Mnyika wakiwa kama mashahidi wangu kwenye kesi ya uhaini wamezuiwa kuingia?

Ntamamiro: Hawawezi kuingia

Jaji: Hilo la kwamba huwezi kuruhusu umelitoa wapi? Kuna amri yoyote ya Mahakama?

Ntamamiro: Siwezi kuwaruhusu.

Jaji Mruma: Tumefikia huko. Unaiambia Mahakama kuwa huwezi kuruhusu na hauna amri yoyote ya Mahakama? Uko serious kweli au hujaelewa ili tufanye maamuzi na sisi sasa?

Ntamamiro: Waheshimiwa majaji naomba radhi.

Katika dodoso lake Lissu alijaribu kuonesha utofauti unaokuwa pale mawakili wa serikali wanapotembelea magereza na mawakili binafsi, ambapo ameonesha kwa mawakili binafsi kumekuwa na upekuzi na kufuatiliwa kwa karibu huku kwa mawakili wa serikali jambo hilo likiwa halipo, hoja ambayo Mkuu wa Gereza aliikanusha.

Lissu alimshutumu Mkuu huyo wa Gereza kuendeshwa na rimoti ya wanasiasa na Kamishana wa Magereza akitoa mifano alipokuja mumbe wa Jumuiya ya Madola, Rais Lazarus Chakwera, Lissu alieleza kuwa alichukuliwa na kupelekwa mjini kukutana naye. Vivyo hivyo alivyokuja Katibu Mkuu wa Umoja wa Mabunge Duniani,  Martin Chungong, Lissu alieleza kuwa alipelekwa mjini kwenda kukutana naye. Hata hivyo Mkuu huyo wa Gereza alikanusha kuwa Lissu alipelekwa kuonana na wajumbe hao. Katika taarifa rasmi, Jumuiya ya Madola na Umoja wa Mabunge Duniani wote wamethibitisha kukutana na Lissu.

Kesi hiyo itaendelea Julai 23, 2026, ambapo kwa upande wa Jamhuri na wajibu maombi wengine watapata wasaa wa kumuuliza maswali shahidi huyo pekee kwa upande wa Jamhuri.

Journalism in its raw form.

The Chanzo is supported by readers like you.

Support The Chanzo and get access to our amazing features.
Digital Freedom and Innovation Day
The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on Saturday April 20, 2024 at Makumbusho ya Taifa.

Register to secure your spot

Did you enjoy this article? Consider supporting us

The Chanzo is supported by readers like you.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Posts

×