The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on April 20, 2024. Register Here

Kwa Wanachama Wenzangu wa CCM, Kuna Maisha Baada ya Mchujo

Kuna heshima katika kubaki mwaminifu, hata kama hukupita. Kuna thamani kubwa katika kuwa sehemu ya chama kikongwe, hata bila cheo.

subscribe to our newsletter!

Katika kila msimu wa uchaguzi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), mojawapo ya hatua muhimu inayozua hisia kali ni mchujo wa wagombea kwenye kura za maoni za chama hicho tawala kupata wagombea watakaopeperusha bendera ya chama kwenye ngazi mbalimbali, ikiwemo udiwani, ubunge, uwakilishi, na hata urais. 

Hiki ni kipindi kinachojazwa na matumaini, matarajio, na wakati mwingine sintofahamu. Watu wenye nia njema na uzalendo wa kweli hujitokeza kwa wingi kutangaza dhamira ya kukiwakilisha chama kwenye vinyang’anyiro hivi vya kulitumikia taifa kupitia nafasi mbalimbali za uongozi. 

Wingi wa watu wanaojitokeza kwenye kura hizi za maoni ni ushahidi wa kukua kwa demokrasia ya ndani ya chama. Hata hivyo, kutokana na idadi kubwa ya watia nia na vigezo vya chama vinavyolenga ufanisi, ni wazi kuwa si kila mmoja ataweza kufuzu. 

Hapo ndipo changamoto ya kisaikolojia na kijamii huanza kujitokeza. Wapo ambao hukata tamaa, hujihisi kutengwa, au hata kuingia kwenye msongo wa mawazo baada ya kutopitishwa.

Lakini swali muhimu la kujiuliza ni hili: Je, maisha ya uongozi yanaishia kwenye mchujo?

SOMA ZAIDI: CCM Yavuna Mabilioni. 5,475 Wachukua Fomu za Ubunge na Uwakilishi 

Ni muhimu kutambua kwamba mchujo ni utaratibu wa kawaida katika chama chochote kinachojali nidhamu, maadili na tija. Ni sehemu ya mchakato wa kuhakikisha kuwa wale watakaobeba bendera ya chama ni wale waliokidhi vigezo kwa wakati husika. Kukosa nafasi si hukumu ya kutokuwa na uwezo — bali ni fursa ya kutafakari, kujipanga upya, na kuendelea kushiriki kwenye shughuli nyingine za kijamii na kichama.

Katika jamii yoyote yenye ustaarabu wa kisiasa, ushindi na kushindwa ni sehemu ya maisha. Katika mazingira haya, watia nia wanapaswa kujiandaa kisaikolojia kupokea matokeo ya mchujo kwa utulivu, heshima na ukomavu wa kisiasa. Hili si jambo rahisi, lakini ndilo linalojenga viongozi wa kweli — wale wanaoweza kusimama imara hata pale wanapokosa nafasi.

Katika hali ya kawaida, mtu anaweza kutumia uzoefu wake kuendelea kuwatumikia wananchi kwa njia nyingine: kupitia taasisi za kiraia, kushiriki kampeni, kutoa ushauri, au hata kusubiri fursa nyingine katika uchaguzi ujao. Maisha ya uongozi hayana njia moja tu — na hayako tu kwenye nafasi za kisiasa.

Wito mkubwa unatolewa kwa watia nia, wafuasi wao, na wanachama kwa ujumla, kuheshimu maamuzi ya chama kwa moyo mmoja. Maamuzi hayo yanazingatia maslahi mapana ya chama na Taifa. Kujitokeza kuunga mkono waliopitishwa ni ishara ya uaminifu wa kweli kwa itikadi ya chama, si kwa matamanio binafsi.

Viongozi wa kitaifa wa CCM wamekuwa mstari wa mbele kusisitiza kwamba ushindani wa ndani ya chama haumaanishi uhasama. Kauli mbiu ya kuwa “Wote ni wetu” inapaswa kuungwa mkono kwa vitendo — kwa kuwa wazo la umoja ndani ya CCM limeendelea kulilea Taifa hili kwa zaidi ya miongo sita.

SOMA ZAIDI: Mchakato Uchukuaji Fomu CCM Washika Kasi: Vijana CCM Wajitosa Majimbo ya Mawaziri 

Kwa hiyo, kwa wale wote walioweka jina lao kwenye orodha ya watia nia, iwe wamepitishwa au la — ni vyema wakumbuke: kuna maisha baada ya mchujo. Kuna nafasi nyingine za kulitumikia Taifa. Kuna heshima katika kubaki mwaminifu, hata kama hukupita. Kuna thamani kubwa katika kuwa sehemu ya chama kikongwe, hata bila cheo.

Uzalendo wa kweli haupimwi kwa idadi ya kura, bali kwa namna unavyoitumikia jamii yako hata bila shinikizo wala sifa. CCM inaendelea — na wanachama wake wote, waliopitishwa na waliokosa, wana wajibu wa kuhakikisha chama kinabaki imara, kikiwa kielelezo cha umoja, uadilifu na maendeleo ya Taifa.
Ahmed Sagaff ni kada wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na mtia nia wa ubunge kupitia chama hicho jimbo la Dodoma Mjini. Kwa mrejesho, anapatikana kupitia musakurusumu1@gmail.com au +255 744 092 763. Haya ni maoni binafsi ya mwandishi na si lazima yaakisi mtazamo wa The Chanzo. Ungependa kuchapisha kwenye safu hii? Wasiliana na wahariri wetu kupitia editor@thechanzo.com kwa ufafanuzi zaidi.

Journalism in its raw form.

The Chanzo is supported by readers like you.

Support The Chanzo and get access to our amazing features.
Digital Freedom and Innovation Day
The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on Saturday April 20, 2024 at Makumbusho ya Taifa.

Register to secure your spot

Did you enjoy this article? Consider supporting us

The Chanzo is supported by readers like you.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Posts

×
×