The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on April 20, 2024. Register Here

Search
Close this search box.

Uchambuzi Bajeti Wizara ya Afya Kwa Mwaka 2024/25

Mei 13, 2024 Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilijadili na kupitisha bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka 2024/25 jumla ya shilingi trilioni 1.3

subscribe to our newsletter!

Mei 13, 2024 Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilijadili na kupitisha bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka 2024/25 jumla ya shilingi trilioni 1.3 ikiwa ni ongezeko la shilingi Bilioni 76.5 ukilinganisha na bajeti ya mwaka 2023/24, sawa na ongezeko la asilimia 6.

Uchambuzi wetu, unatoa alama katika vipengele mbalimbali vya bajeti kwa madaraja matatu A ikionesha inaridhisha, B inaridhisha ingawa ina changamoto na C ina changamoto  za msingi.

SOMA ZAIDI: Uchambuzi wa Bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Kwa Mwaka 2024/25

Kipengele cha kwanza tulichoangalia ni eneo la upelekaji fedha iliyotengwa kwenye bajeti. Katika eneo hili, tumeipatia Wizara ya Afya alama A. Katika kipindi cha miaka mitatu 2020/21 hadi 2022/23 Wizara ya Afya imekuwa ikipokea fedha kwa zaidi ya asilimia 88.

Mwaka 2021/22 wizara ilipokea fedha kwa asilimia 130 kutokana na nyongeza ya bajeti iliyotokana na fedha za mkopo za kukabiliana na athari za UVIKO-19.

Hata hivyo, kwa mwaka 2023/24 hadi kufika mwezi Machi 2024 wizara ilipokea kiasi cha shilingi bilioni 838 sawa na asilimia 68 ya bajeti ikiwa imebaki miezi mitatu kumaliza mwaka wa fedha husika. Jambo hili linatia wasiwasi kama wizara hii itaweza kupatiwa fedha ilizoidhinishwa na bunge zaidi ya 88%.

Eneo la pili tuliloangalia ni eneo muundo wa taarifa ya wizara ya bajeti. Katika eneo hili tumeipa alama A kutokana na namna ambavyo taarifa hiyo imeweza kuainisha vipaumbele vya Wizara na afua zake pamoja na kiwango cha fedha kilichotengwa katika kutekeleza kipaumbele husika. Uwasilishaji huu wa taarifa unasaidia wananchi kuelewa vipaumbele gani vimepatiwa fedha zaidi wakilinganisha na mahitaji yao.

SOMA ZAIDI: Uchambuzi Bajeti ya TAMISEMI 2024/25

Baadhi ya vipaumbele hivyo ni pamoja na kuimarisha huduma za kinga dhidi ya magonjwa, kuimarisha mifumo ya ugharamiaji wa huduma za afya nchini, kuimarisha huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto ili kupunguza vifo vya wajawazito na watoto wachanga na kuimarisha upatikanaji na ubora wa huduma za afya zinazotolewa na vituo vya kutolea huduma za afya kuanzia ngazi ya Zahanati hadi Taifa.

Changamoto kubwa katika muundo wa taarifa ya bajeti ya wizara ni mchanganuo wa matumizi mengineyo ambayo yanaonekana kuwa makubwa sana ukilinganisha na baadhi ya wizara nyingine za huduma za jamii.

Eneo la tatu ni eneo la mrejesho wa bajeti iliyopita, yaani taarifa ya utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2023/24. Katika eneo hili, tumeipatia Wizara ya Afya alama A kutokana na namna ambavyo wizara imeweza kutoa mrejesho wa utekelezaji wa bajeti kwa kuzingatia vipaumbele vya Wizara na utekelezaji wa taasisi na mamlaka mbalimbali zilizochini yake.

SOMA ZAIDI: Uchambuzi: Bajeti ya Wizara Ya Nishati 2024/25 Ni Ndogo Zaidi Kutokea Katika Kipindi Cha Miaka Mitano. Hiki Ndicho Kilichosababisha

Mrejesho huo wa Wizara pia umehusu taarifa muhimu za hali ya afya za wananchi kwa ujumla. Mfano wa taarifa za wa wagonjwa wa ndani na nje katika kipindi cha Julai 2023 mpaka Machi 2024, wagonjwa wa magonjwa yasiyoambukizwa, watumiaji wa uzazi wa mpango, na taarifa nyingine nyingi muhimu ambazo zinaweza kuwasaidia wananchi na wadau mbalimbali wa masuala ya afya.

Eneo la nne tuliloliangalia ni eneo la watumishi wa afya nchini. Kwa mujibu wa Wizara mahitaji halisi ya watumishi wa afya nchini ni 348,923, lakini hadi Machi mwaka huu kulikuwa na watumishi wa afya 126,925 katika ngazi ya afya ya msingi na hospitali za rufaa za mkoa, kanda na taifa. 

Katika eneo hili tumeipa alama C wizara ya afya kwa sababu licha ya upungufu huo mkubwa wa watumishi, kwa mwaka 2023/24 taarifa ya wizara inaonesha Serikali imetoa vibali vya ajira za watumishi wa afya 13,187 tu, na kwa mwaka 2024/24 taarifa ya Wizara haijaeleza kwa kina ni ajira ngapi zimepangwa kutolewa ili kukabiliana upungufu.

SOMA ZAIDI: Uchambuzi: Bajeti ya Wizara ya Kilimo 2024/25 Inaakisi Umuhimu wa Sekta ya Kilimo?

Hali hii inafanya upungufu wa watumishi wa afya nchini kuwa kwa asilimia asilimia 64 ni changamoto kubwa kwa ustawi wa wananchi na itaichukua nchi miaka mingi  kuweza kuziba hili ombwe hili kama jitihada za maksudi hazitafanyika, licha ya Serikali kuendelea na juhudi za ujenzi wa vituo vya kutolea huduma.

Eneo la tano tuliloliangalia ni eneo la bima ya afya ambalo tumelipa alama C. Hivi sasa taarifa ya wizara inaonesha kuwa ni asilimia 15 tu ya watanzania ndio wamejiunga na Mifumo ya Bima za Afya. Kati ya hao wanufaika wa NHIF asilimia 8, CHF na Bima Binafsi asilimia 7.

Hata hivyo, suluhisho la changamoto ya wananchi na Serikali kugharamia huduma za afya ilionekana ni kupitia kuanzishwa kwa mfuko wa bima ya afya kwa wote. Serikali ilitunga Sheria namba 13 ya mwaka 2003 ya bima ya afya kwa wote. Lengo likiwa ni kuhakikisha kila mtanzania anakuwa na bima ya afya.

Matarajio yalikuwa ni katika bajeti ya mwaka wa fedha 2024/25 Serikali itakuja na taarifa ya kukamilisha mchakato wa bima ya afya kwa wote ikiwemo kufanya tathmini ya vyanzo na viwango vya fedha kwa ajili ya mfuko wa kugharamia watu wasio na uwezo kupitia Sheria ya Bima ya Afya kwa wote.

Lakini katika taarifa ya Wizara ya bajeti kwa mwaka 2024/25 hakuna maelezo ya kina yaliyotolewa juu ya tarehe mahususi ya kuanza kwa bima ya afya kwa wote, badala yake Serikali imetoa maelezo ya kuahidi kuendelea na ukamilishaji wa mchakato huo.

Digital Freedom and Innovation Day
The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on Saturday April 20, 2024 at Makumbusho ya Taifa.

Register to secure your spot

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *