The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on April 20, 2024. Register Here

Search
Close this search box.

Ufafanuzi Mdogo Kuhusu Kikokotoo Kipya cha Asilimia 33

Siyo kweli kwamba kikokotoo hicho kinapunguza mafao kwa mnufaika.

subscribe to our newsletter!

Kumekuwepo na hofu kubwa miongoni mwa wafanyakazi tangu kikokotoo kipya katika mifuko ya hifadhi ya jamii nchini kianze kutumika hapo Julai 1, 2022. Kikotoo hicho ni matokeo ya makubaliano ya pamoja kati ya Serikali, Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA) na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE).

Moja kati ya malalamiko makubwa kuhusiana na kikokotoo hicho ni madai kwamba Serikali imeamua kupunguza malipo kwa wastaafu, huku wakosoaji wakitaja kushuka kwa malipo ya kiinua mgongo kutoka asilimia 50 mpaka asilimia 33 kama ushahidi wa malalamiko yao hayo.

Licha ya kikokotoo hicho kufanya kazi kwa takriban mwaka mmoja sasa, bado malalamiko yameendelea kuwepo miongoni mwa wafanyakazi na wastaafu, hali iliyoisukuma TUCTA kujitokeza hadharani hivi karibuni na kuitaka Serikali itoe elimu zaidi kuhusiana na suala hilo nyeti.

Akizungumza mjini Morogoro hapo Machi 9, 2023, Rais wa TUCTA Tumaini Nyamhokya alisema kwamba moja kati ya makubaliano yao na Serikali ni kwamba Serikali ihakikishe inatoa elimu ya kutosha kwa wafanyakazi ili waelewe kikokotoo hiki kipya ni nini.

Mimi siyo mtu wa Serikali lakini nikiwa kama mtaalam wa masuala ya hifadhi ya jamii nimehisi kuwiwa kutoa mchango wangu ikiwa ni sehemu ya kusaidia juhudi hizi za kuelimisha umma kuhusiana na jambo hili muhimu kwa ustawi wa wafanyakazi, wastaafu, na taifa kwa ujumla.

Usalama wa kifedha

Ni muhimu kwanza tukafahamu kwamba mfumo wa hifadhi ya jamii, ambao hufadhiliwa na wanachama wa mfuko husika kwa njia ya michango ya kila mwezi, hulenga kuhakikisha kuwa wanachama wanapata huduma za kijamii kama vile afya, elimu, pensheni, na huduma nyingine za kijamii.

Mbali na malengo hayo, hifadhi ya jamii pia huhakikisha usalama wa kifedha kwa wanachama wake pindi mwanachama apatapo janga lolote litakalosababisha yeye kupoteza kipato, ikiwemo kustaafu, ulemavu, kufiwa, uzazi, na kukosa ajira.

Kwenye fao la pensheni, mfuko hutumia zana maalum kuhesabu kiasi cha pensheni ambacho mwanachama atapokea baada ya kustaafu. 

SOMA ZAIDI: Kwa Nini Inachukua Muda Mwingi Kwa Watu Kupata Mafao Yao Kutoka NSSF, PSSSF?

Zana hii huzingatia mambo mbalimbali kama vile muda wa kuchangia, kiwango cha michango ya kila mwezi, kiwango cha riba kinachopatikana, na muda wa malipo ya pensheni. 

Kwa kutumia taarifa hizi, zana hii inaweza kutoa makadirio ya kiasi cha pensheni ambacho mwanachama atapokea baada ya kustaafu. Hii zana ndiyo huitwa kikokotoo.

Ulipaji

Kwenye malipo ya pensheni, mnufaika hulipwa kwa awamu mbili: awamu ya kwanza inaitwa mkupuo, au kiinua mgongo, na awamu ya pili ndiyo wengi tunaifahamu inaitwa pensheni ya mwezi ambapo mnufaika hupokea malipo ya pensheni kila mwezi.

Nataka niseme hapa kwamba siyo kweli kwamba kiwango cha pensheni kimepanda au kimeshuka kwa mnufaika tangu Serikali itangaze matumizi ya kikotoo kipya hapo Julai 2022. 

Kilichobadilika baada ya kutangazwa kwa kikotoo hicho ni njia za kukokotoa haya malipo katika awamu zote mbili za malipo, yaani kiinua mgongo na malipo ya kila mwezi.

Zamani kabla ya hiki kikokotoo kipya cha asilimia 33, mnufaika wa pensheni alikuwa analipwa asilimia 25 katika malipo ya mkupuo, yaani malipo ya awamu ya kwanza, kwa kutumia kanuni ya CP = (1/580*N*APE) *12.5*25%) na malipo ya awamu ya pili akilipwa asilimia 75 kwa kutumia kanuni ya MC = (1/580 * N*APE)*75%*1/12).

Kilichobadilika ni kwamba sasa hivi mnufaika wa pensheni atakuwa analipwa kiinua mgongo, yaani malipo ya awali, asilimia 33 kutoka asilimia 25 na malipo ya kila mwezi atakuwa analipwa asilimia 67 kutoka asilimia 75.

Kwa hiyo, tunaweza kuona hapa kwamba kilichoongezeka ni malipo ya awali huku malipo ya kila mwezi yakipungua. Lakini malipo kwa ujumla yako vilevile, yaani asilimia 100 (33 + 67 = 100) kama inavyoonekana hapo juu.

Mnufaika alipwe pesa zote?

Kwa mtazamo wangu, faida moja wapo ya kikokotoo hiki kipya ni kwamba mnufaika wa pensheni atalipwa kiinua mgongo kikubwa tofauti na zamani, na hivyo kumfanya kuwa na uwezo mkubwa wa kuwekeza na kufanya mambo yake mengine baada ya kustaafu.

Nafahamu baadhi ya madai ambayo yamekuwa yakitolewa na wafanyakazi, wastaafu, na wadau wengine wakishinikiza walipwe pesa zao zote baada ya kustaafu. 

Hata hivyo, nasikitika kuhitimisha kwamba jambo hili ni gumu kulitekeleza kwani siyo tu lipo nje ya sheria na miongozo ya hifadhi ya jamii Tanzania bali pia ni kwenda kinyume na dhana nzima ya hifadhi ya jamii.

SOMA ZAIDI: Kwa Nini Ni Muhimu Kufungamanisha Bima ya Afya na Hifadhi ya Jamii?

Duniani kote, pia, hakuna sehemu ambako utaratibu kama huo unatumika.

Nihitimishe safu hii kwa kukumbusha kwamba lengo kubwa la pensheni ya kustaafu/uzee ni kukulinda/kumlinda mnufaika wa pensheni kwenye kipindi chote cha uzee mpaka pale atakapo kufa.

Zipo hasara nyingi za kiuhifadhi wa jamii endapo kama wanufaika watalipwa malipo yao yote kwa asilimia 100, kwa ujumla, pale anapo staafu. 

Hizi ni hasara zinazogusa pande zote, mfuko husika na mnufaika pia!

Thomas Ndipo Mwakibuja ana shahada ya sayansi kwenye hifadhi ya jamii kutoka Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM). Kwa maoni, anapatikana kupitia thomasmwakibuja@gmail.com au +255 767 879 281. Haya ni maoni binafsi ya mwandishi na si lazima yaakisi mtazamo wa The Chanzo Initiative. Unataka kuchapisha kwenye safu hii? Wasiliana na wahariri wetu kupitia editor@thechanzo.com kwa maelekezo zaidi.

Digital Freedom and Innovation Day
The Chanzo is hosting Digital Freedom and Innovation Day on Saturday April 20, 2024 at Makumbusho ya Taifa.

Register to secure your spot

22 Responses

  1. Kwani ni sababu Gani za msingi zilizosababisha kubadilisha kikokotoo na kuacha Cha zamani Ili Hali hakuna mnufaika aliyelalamika? Pia hakuna sababu za msingi zaidi yamunufaa yenu binafsi baadae ya kuona mmemaliza hela kwenye majumba yasiyouzika na hamna kitu.Turudishieni kikokotoo Cha zamani msijitetee kujifanya mnajua kukokotoa wakati mlifeli hesabu.

  2. Bwana Thomas Mwakibuja, ufafanuzi wako ni mzuri, ila kama mwana-mahesabu sijajua kwenye kanuni zote ulizotuwekea kwenye maelezo hazieleweki kwa sababu; kuna variables hujazisema zina maanisha nini katika kanuni zote mbili za kikokotoo cha mkupua (kiinua mgongo na kile cha pensheni ya kila mwezi)! Kwa sisi wastaafu tunataka tujua tutatoka mzigo kiasi gani? Ahsante.

  3. Umeeleza vizuri sana ila hizo fomla zako hazijaeleweka ni vema ukaeleza maana ya izo symbo uchanganuz wa kanuni.

  4. Kikokotoo kina mazuri yake na mapungufu yake.
    MAZURI:
    Kuweka uwiano sawa wa malipo kwa watumishi wote tofauti na pale zamani kulikuwa na wafanyakazi wengine walikuwa kidogo na wengine wanalipwa kiwango kikubwa, HIli mimi naona ndiyo nzuri pekee kwemye kikokotoo hiki kpya
    MAPUNGUFU:
    Kikokotoo kipya ubaya wake ni kanuni (Formular) inayotumika, kuna tarakimu zimeondolewa na zingine kuwekwa ambazo zinapelekea malipo ya mkupuo yawe kidogo. Mfano kwenye kanuni (formular) kutoa 540 ilipokuwa na kuweka 580, na kuondoa 15 ilipokuwa kwenye kanuni na kuweka 12.5, vile vile kuondoa 50% na kuweka 33%. Pia kutumia wastani wa mishahara ya miaka mitatu katika kukokotoa badala ya kutumia mshahara wa mwisho. Haya yamepelekea malipo ya mkupuo kuwa kidogo

    HOJA
    1. Kuwa kiongozi siyo kuwa una akili nyingi kuliko unao waongoza, uongozi ni ukilanja tu kwa kipindi hicho kwa sababu wote hatuwezi kuwa viongozi kwa wakati mmoja. Kiongozi anaejisikia hivyo huyo hafai kuwa kiongozi
    2. Michango ya mtumishi ni hela yake mwenyewe kwanini umpangie namna ya kutumia hela hiyo?
    3. Mfuko wa hifadhi ya jamii (PSSSF) huwekeza ili kulinda thamani ya pesa, na kuwekeza maana yake ni kuzalisha pesa, iweje mwisho wa siku malipo yawe duni wakati pesa ilikuwa inazalisha? Ukiona hivyo ujue kuna uwekezaji usio na tija. Ndiyo maana tunaambiwa mfuko utafilisika, hii haiingii akilini. Kama hoja ni hiyo, kwanini asiulizwe Rais wa awamu ya nne Mh. Kikwete, mbona yeye alikuwa analipa vizuri na hatukusikia mifuko imefilisika? na bahati nzuri yupo hai, mwenyezi Mungu aendelee kumjalia afya njema.
    4. Mtumishi wa umma mwaajiri wake ni taasisi ya serikali, na PSSSF ni taasisi ya serikali, usipo mlipa vizuri mstaafu lawama zote zitaelekezwa serikalini matokeo yake mwaajiri mkuu wa utumishi wa umma ndiyo anabeba lawama zote hizo.
    5.Kustaafu siyo dhambi, lakini kwa malipo haya kustaafu ni dhambi, mstaafu inakuwa hathaminiwi, Lakini mtumishi huyo huyo ndiyo jamii ya watekeleza sera za Nchi kwa mstakabali wa maendeleo ya Nchi
    6. Ukipitia annual report ya CAG kwenye kipengele cha taasisi za umma na Annual report PSSSF hapo unaona yanayosemwa na wasemaji na yaliyofanyika na watendaji. Hivyo tunakiona kinachoendelea., Upo?
    HITIMISHO
    Mstaafu alipwe mafao yake kwa kuboresha kikokotoo hiki kwenye kanuni (Formualar), hiyo ni haki yake.

    1. Ndugu inaonekana una uelewa wa hii kitu umemanisha nini kusema wastaafu wote watapewa sawa tofauti na zamani?
      Mfano- Kuna kijana alibaatika kuajiriwa akiwa na miaka 27
      Na mwingine akachelewa akaajiriwa na miaka 40
      Na wakastaafu wakiwa daraja mfanano.
      Je! malipo Yao yatafanana?

  5. SHUKRAN:
    KIKOKOTOO KIPYA KINAPUNJA HAKI YA MSTAAFU NI KINAMFANYA KUPATA MALIPO MADGO, KWENYE 15.5 IMEKUWA NI 12.5 HHII 3 NI PESA KUBWA KWAKE, NA ILE 1/540 IMEKUWA NI 1/580 ukifanya diduction mathematically utaona pengo hapo wewe TUCTA NA ATE mnafaida si bure natamani kusema ni kumuibia marehemu unamkadiaje mtu umri wa kuishi wa miaka 12? wewe umeongea na MUNGU au una ujomba nae, wapeniwastaa haki zao

  6. Kila badiliko lililofanywa ni kwa nia ya kumpunja mstaafu.
    1. Badala ya 1/540 imewekwa 1/580 ili kumpunja mstaafu. Maana yake ni kwamba badala ya kugawa kwa 540 wamegawa kwa namba kubwa 580 ili kupata jawabu DOGO au kiinua mgongo KIDOGO.
    2. Badala ya kuzidisha kwa 15.5 wanazidisha kwa namba ndogo 12.5 ili kupata jawabu DOGO au kiinua mgongo KIDOGO.
    3. Kwa PSPF iliokuwa inazidishwa kwa 50% sasa wanazidisha kwa 33% ili kupata jawabu DOGO au kiinua mgongo KIDOGO.
    Mabadiriko yote matatu hapo juu yanalenga kumpunja mstaafu.
    Kwa hiyo kustaafu kuanzia kipindi cha awamu ya tano ya serikali ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania imekuwa kama ni adhabu waliotangulia wanafurahia maisha wengi walishawekeza kwenya mahati fungani pesa iliyobaki baada ya kurekebisha mambo muhimu. Wanaostaafu sasa hivi hawawezi kurekebisha chochote wala kuwekeza, akienda benki inawezekana kabisa kuchukua kiinua mgongo chote na kikatosha kukarabati nyumba tu.

  7. Kwa malipo ya mafao ya wastaafu kwa kikokotoo hiki kipya naungana na mwaandishi wa kitabu cha literature “NOT YET UHURU” (by Ngugi Wathiong’i) back ground yake ni Kenya. Kinaeleza hivi: Wale waliokuwa mstari wa mbele kumtoa mkoloni ili Nchi iwe huru baada ya zoezi hilo kuisha waliporudi nyumbani waliwakuta wale waliowaacha ndiyo wameshika madaraka/ wamekuwa watawala, wakawa wanawatumikisha ovyo ovyo tena zaidi hata ya kipindi cha wakoloni, Ndipo waliokuwa mstari wa mbele wakawa wanajiuliza hivi kweli tuko huru tumepata uhuru? mbona imekuwa zaidi ya awali! Hali hii bado hatuko huru ndiyo maana ya NOT YET UHURU. Mstaaafu ndiyo aliyetekeleza sera kwa vitendo kwa mstakabali wa maendeleo ya Nchi, lakini hawathaminiwi, wanathaminiwa wanaopiga makelele muda wote. Hii si sahihi kabisa, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema Nchi hii ni yetu sote, lakini katika hili? Nchi hii ina wenyewe. Wastaafu hawana lakufanya kwasababu wameshika makali na hao wapiga kelele ndiyo wameshika mpini,
    Wastaafu Mungu yupo atawapigania tu na Mungu anafursa nyingi atawalipeni haki zenu!

  8. naomba kujifunza zaidi.Hivi ikitokea mstafu amekufa zile hela zake zilizobaki inakuwaje? wanapewa ndugu zake au NSSF wanazigawana ? au serikali inazichukua?

    1. Inategemeana mstaafu amefariki ndani ya muda ule wa miaka 12.5 au amefariki akiwa nje ya muda alokadiriwa, ikiwa amefariki ndani ya miaka 12.5 wategemezi wake wanaweza kudai kiasi cha fedha kilichobakia ambacho marehemu angepokea ndani ya miaka 12.5,lkn kama alishavuka miaka 12.5 hatolipwa maana alikuwa anachukua ziada ya mfuko wa hifadhi ya jamii na hii ndo siri-kali ilipo..!!! maana ni wachache wanaovuka miaka hiyo kwa sababu kuna baadhi ya watumishi kutoboa 60 tuu ni shughuli na mchakato wa kudai wenyewe unakuchosha

  9. ni kweli kwamba wastafu wengi wakipewa hela wanazitumia vibaya aidha kwa sababu wakupewa elimu tosha ya matumizi ya fedha ya kustafu.sasa kwa mfano ikatungwa sheria kwa ,hela za kustafu ziwekwe directly kwenye bank za kibiasha ambazo zinatoa gawio kila mwezi ,si itakuwa nafuu kuliko hiyo pesheni ya kila mwezi anayopewa mstafu ?

  10. Kiukweli kikokotoo mmefeli sana tu mtu analipwa million 9 kweli na amesomesha kwa madeni zaidi ya hizo pesa wanalipaje na bado wameuza hadi aridhi zao kisa mishahara mibovu wakitengemea good future kweli serikali na huu mfumo na hamuwapendi watu. Sawa endeleeni kwa kuona munaongoza wasio na hakili 😭😭😭😭

  11. Kikokotoo ni kitanzi Kwa wastaafu kwani wastaafu wengine wanategemea malipo ya mkupuo kutekeleza mipango Yao ya uzeeni.makato yalipoanza hamkusema Kuna mipangilio yenu lakini Hela imeiva mnatupangia huo ni unyonyaji. Nipeni Hela yangu nikatekeleze mipango yangu.

  12. Inasikitisha kuona, badala ya kukokotoa wakitumia mshahara wako wa mwisho, wanatumia wastani wa miezi 36 ili tu mstaafu huyo wamnyonye.
    Hii ni kumuua mstaafu mapema na wala sio kumsaidia.

  13. Think twice of this
    Ni kwamba hujatakatu ww kustaff ndo maana changamoto huwezi kuzielewa vizuri
    Fanyeni jambo
    Sio watu wajutie kufanya kaz
    😢😢

  14. Tatizo kubwa ni kanuni, 1/540 kuwa 1/580; 15.5 kuwa 12.5 na kuondoa mshahara wa mwisho na kuweka wastani wa mishahara miezi 36. Vyote hivi vimechangia sana kupunguza jibu la mwisho. Ni shida!

  15. Kiukweli kwa kikokotoo hiki kipya, Wengi tutakufa mapema tu kwa stress tu, maana unajikuta mpaka unastaafu na mishahara yetu hii midogo hujafanya lolote wala chochote. yani bado unasomesha na bado wategemezi kibao wanakutegemea maana walau kama wangetoa 50% kwa mkupuo wengine tungeweza ata kuwaachia wategemezi walau kibanda tu cha kuishi wao ili juepukana na KODI za mapango.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *